HIYO ni kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Kazi la Umoja wa Mataifa (ILO), ikieleza namna mazingira ya kazi yanavyoweza kuhatarisha afya na kusababisha kifo kwa mwajiriwa.
Iko hivi; kwa mujibu wa ILO, watu zaidi ya 840,000 hupoteza maisha kila mwaka kutokanana na mazingira yao ya kazi.
Katika ripoti hiyo, ILO imesema mazingira yanayoweza kuharibu afya na hata kusababisha kifo cha mwajiriwa ni pamoja na kufanya kazi muda mrefu, kutokujua hatima yake, malipo kiduchu yasiyoendana na jitihada zake, na hata manyanyaso ya bosi wake.
Utafiti wa ILO umefafanua kuwa asilimia 35 ya waajiriwa duniani kote hufanya kazi kwa saa zaidi ya 48 kwa wiki.
Kama hiyo haitoshi, asilimia 23 wameshawahi kukumbana na msongo wa mawazo kutokana na manyanyaso kutoka kwa waajiri wao.
Kwa mujibu wa ILO, mazingira ya aina hiyo huathiri afya ya mwajiriwa, ikiwamo kumsababishia msongo wa mawazo unaoweza kuzalisha shinikizo la damu, magonjwa ya moy o, kiarusi, na hata kujiua.
“Hatari za kisaikolojia zimekuwa moja ya changamoto kubwa katika maeneo mengi ya kazi,” amesema Kiongozi wa Timu ya Mifumo ya Usalama wa Maeneo ya Kazi wa ILO, Manal Azzi.
“Kuna umuhimu mkubwa wa kuboresha saikolojia katika mazingira ya kazi, si tu kwa ajili ya kuwalinda waajiriwa, bali pia itaongeza uzalishaji, kuboresha utendaji wa taasisi na kuongeza uchumi.”






