KWA mara ya kwanza katika historia ya Uingereza, idadi ya wanawake wanaofanya upasuaji wa kupunguza ukubwa wa matiti imekuwa kubwa kuliko ya wanaoongeza.
Hilo limethibitishwa na utafiti wa Chama cha Wataalamu wa Upasuaji wa Kubadili Mwonekano nchini humo (BAAPS).
Katika ripoti yao, watafiti wa BAAPS wamebaini kuwa matukio ya kuongeza ukubwa wa matiti yalipungua kwa asilimia 8 mwaka 2025.
“Kwa mwaka 2025, ni matukio 4,761 pekee, sawa na upungufu wa asilimia 8, ukilinganisha na takwimu za mwaka 2024,” imeeleza ripoti ya BAAPS.
Akizungumza matokeo ya utafiti wao, Rais wa BAAPS, Nora Nugent, amesema: “Kwa mara ya kwanza, tumeshuhudia ongezeko kubwa la upasuaji wa kupunguza ukubwa wa matiti.
“Wagonjwa wengi (waliopunguza ukubwa wa matiti), wameeleza sababu kuwa ni kutaka uhuru zaidi wakiwa wanafanya mazoezi.
“Wengine wanasema ukubwa wa matiti unawafanya washindwe kuvaa baadhi ya nguo wanazozipenda.”
Aidha, watafiti wa Chama hicho wamegundua ongezeko la asilimia 27 la matukio ya upasuaji wa kurekebisha mwonekano wa uso.
Katika hatua nyingine ya utafiti, BAAPS wameeleza kuwa bado wanawake ndiyo wateja wakubwa wa upasuaji wa kubadili mwonekano, ikiwamo kuongeza au kupunguza ukubwa wa matiti na makalio.
“Katika matukio yote 25,217 ya mwaka 2025, asilimia 93.9 ni wanawake. Hata hivyo, idadi imepungua kwa asilimia 2, ukilinganisha na mwaka 2024,” imeeleza ripoti ya utafiti huo.






