Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, ametangaza kuanza kwa maboresho makubwa katika Uwanja wa Benjamin uliopo jijini Dar es Salaam.
Kupitia kwenye ukurasa wake wa Instagram, Msigwa amesema kuwa marekebisho hayo yanahusisha sehemu ya kuchezea (Pitch), ambayo inatarajiwa kuwa ya kisasa ndani ya kipindi cha miezi sita ijayo.
Amesema lengo ni kuwa na pitch yenye viwango vya juu vya Kimataifa, sambamba na kuboresha maeneo mengine ya uwanja ikiwemo lounges, vyumba vya kubadilishia nguo (changing rooms), ubao wa matokeo (Scoreboard) pamoja na mwonekano wa jumla (Branding).
Aidha, ameomba radhi kwa mashabiki wa soka kwa kutoweza kuutumia uwanja huo katika dabi ya Kariakoo iliyopangwa kufanyika Mei 3, 2026, akiahidi kuwa baada ya maboresho kukamilika, uwanja huo utakuwa katika hali bora zaidi kwa matumizi ya muda mrefu.










