Msafara wa magari wenye mwili wa Hayati Rais Dk. John Magufuli ukiingia Uwanja wa Jamhuri kwa ajili ya mazishi ya kitaifa.
NA RIPOTA WA PANORAMA
HAYATI Rais Dk. John Pombe Magufuli, aliyefariki dunia Machi 17, 2021 katika Hospitali ya Mzena jijini Dar es Salaam, leo ameagwa na wananchi wa Mkoa wa Dodoma na mikoa ya jirani katika Uwanja wa Jamhuri.
Wananchi wa Dodoma na mikoa ya jirani wamepata nafasi na kumuaga Hayati Rais Dk. Magufuli katika mazishi ya kitaifa yaliyoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan na kuhudhuriwa na marais na wakuu wa nchi 17, viongozi wa mashirika ya kimataifa, marais wastaafu wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi na Dk. Jakaya Mrisho Kikwete pamoja na viongozi wa kitaifa.
Mwili wa Hayati Rais Dk. Magufuli umewafikishwa katika Uwanja wa Jamhuri Dodoma majira ya saa nne na dakika arobaini asubuhi lakini wananchi wa Dodoma na mikoa ya jirani walianza kufika uwanja hapo mapema asubuhi
Janeth Magufuli, mjane wa Hayati Rais Dk. John Pombe Magufuli akiwa ameghubikwa na huzuni wakati wa mazishi ya kitaifa ya mumewe.
Mazishi hayo ya kitaifa yalitanguliwa na sala kabla ya Rais Samia, Janeth Magufli (mjane ya Hayati Rais Dk. Magufuli) marais na viongozi wa mataifa mbalimbali ya Afrika kutoa heshima za mwisho mbele ya jeneza lililokuwa na mwili wake.
Baada ya shughuli hiyo, gari maalumu la kijeshi lililokuwa na mwili wake lilizunguka mara tano katika Uwanja wa Jamhuri kwa ajili ya kuwapa wananchi fursa ya kumuaga na baada ya hapo, mwili huo ulipitishwa katika mitaa maarufu ya Jiji la Dodoma iliyokuwa imefurika maelfu ya wananchi waliokuwa wamejipanga kutoa heshima zao za mwisho.
Gari maalumu la kijeshi lililokuwa na mwili wa Hayati Rais Dk. Magufuli lilipita katika mzunguko wa barabara za Bahi na Shule ya Msingi Uhuru, Barabara ya Iringa, Mirembe Hospitali, Barabara ya Kigamboni, mzunguko wa Jamatini, Bunge, Emmaus ya Pili mpaka mataa, Barabara ya Mataa kuelekea makazi ya Waziri Mkuu, African Dream kuelekea njia panda ya wajenzi hadi uwanja wa ndege.
Wananchi wa Dodoma wakiwa wamejipanga barabarani kuuaga mwili wa Hayati Rais Dk. Johm Pombe Magufuli.
Wananchi wa Dodoma wakiwa katika Uwanja wa Jamhuri wakati wa mazishi ya kitaifa ya Hayati Rais Dk. John Pombe Magufuli