DAR ES SALAAM:
TUME ya kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani yaliyojitokeza wakati na baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, Februari 24 imekutana na aliyewahi kuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya.
Mahojiano hayo ya tume na Sabaya yamefanyika katika ofisi za tume hiyo zilizopo Benki Kuu ya Tanzania (BoT) mkoani hapa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kukusanya taarifa, maoni na ushauri kutoka kwa watu mbalimbali wakiwemo viongozi wa sasa na wastaafu.
Imeelezwa kuwa tume na Sabaya walijadili kwa kina namna matukio ya uvunjifu wa amani yalivyoanza, athari zake kwa wananchi, mali zao na miundombinu pamoja na ushauri na mapendekezo ya namna ya kudhibiti na kuzuia matukio kama hayo yasijirudie siku zijazo.

Hivi karibuni mamlaka ya uteuzi imeiongezea tume muda wa siku arobaini na mbili (42) kuanzia Februari 20, 2026 ili iweze kukamilisha uchunguzi wa matukio ya uvunjifu wa amani ya wakati na baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, 2025 na kuitaka ikamilishe kazi na kuwasilisha taarifa yake kabla au ifikapo Aprili 3, 2026.

Kwa sasa tume inaendelea na mahojiano na waathirika wa matukio hayo kwa ajili ya hatua zaidi kama taifa ili matukio kama hayo yasijirudie tena
