RIPOTA PANOTAMA
Rais Samia Suluhu Hassan, ametuma salamu za rambirambi kwa kifo cha Mwadhamu Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bakari Machumu, Kardinali Pengo alifariki dunia usiku wa Februari 19, 2026, katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es Salaam.
Taarifa ya Machumu inaeleza kuwa Rais Samia amepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za kifo hicho na kumuelezea Kardinali Pengo kama kiongozi wa kiroho na mzalendo aliyetoa mchango mkubwa katika kuimarisha imani, maadili, umoja na mshikamano wa kitaifa.
Kwamba kwa muda wote wa uongozi wake wa muda mrefu ndani ya Kanisa Katoliki, Kardinali Pengo alisimama imara kuhubiri amani na maadili mema na hivyo kuacha alama isiyofutika katika jamii.
“Taifa limepoteza kiongozi aliyelitumikia kwa uadilifu na kujitolea. Mchango wake katika malezi ya kiroho na maadili utaendelea kukumbukwa, kuthaminiwa na kuenziwa,” amesema Rais Samia.
Rais amemtumia salamu za pole Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi, OFMCap, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), viongozi wa dini pamoja na waumini wote walioguswa na msiba huo.
Aidha, Rais Samia ameungana na kanisa, waumini na watanzania wote katika kipindi hiki cha majonzi na kumuomba Mwenyezi Mungu aipumzishe roho ya marehemu mahali pema peponi.
