RIPOTA PANORAMA
ALIYEKUWA Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Polycarp Kardinal Pengo, amefariki dunia Februari 19, 2026 majira ya saa nne usiku.
Taarifa za kifo chake ilitolewa jana usuki na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Thaddeus Ruwa’ichi kwa waraka wa kanisa uliotumwa kwa makardinali, maaskofu, mapadre, watawa na waumini wote wa kanisa hilo.
Katika waraka huo, Askofu Mkuu Ruwa’ichi amesema Kardinali Pengo alifariki akiwa kwenye matibabu katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es Salaam.
“Ninayo masikitiko makubwa kuwatangazieni kwamba mpendwa baba yetu Mwadhama Polycarp Kardinal Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, ameitwa nyumbani kwa Baba wa Milele akiwa katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es Salaam,” ameeleza Ruwa’ichi
Kuhusu mipango ya mazishi amesema taarifa zitatolewa baadaye baada ya maandalizi kukamilika, huku waamini wakihimizwa kuendelea kumuombea marehemu apumzike kwa amani.
