![]() |
Waziri Mkuu, Kassin Majaliwa |
NA MWANDISHI WETU
WAZABUNI waliosambaza vipuli na kutengeneza magari ya Wizara na Idara za Serikali kupitia Karakana Kuu ya Temesa – MT Depot, wamemuomba Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa aingilie kati kusaidia walipwe madeni wanayodai.
Akizungumza na Tanzania PANORAMA Blog, Mwenyekiti wa Umoja wa Gereji Tanzania (UGETA), Lumona Mkala, alisema wanachama wake wanaidai Temesa – MT. Depot zaidi ya shilingi Bilioni nne.
Mkala amesema kwa nyakati tofauti wamefuatilia kulipwa fedha zao bila mafanikio na wakati mwingine wanapewa majibu yasiyoonyesha ushirikiano kutoka Ofisi ya Meneja wa MT Depot, Injinia Joseph Maronga.
“Unapofika ofisi ya meneja, unaambiwa nenda kwa mhasibu, ukifika kwa mhasibu anakwambia urudi kwa Meneja…Hivyo tunakuwa hatuna majibu ya lini pesa zetu tutalipwa,” amesema Mkala.
Amezitaja baadhi ya gereji zinazodai kuwa ni Beka Investment shilingi 250,563,150, Moroturbo shilingi 80,256,197, Planet Busines link shilingi 175,312,570 na Ndeken shipingi 194,801,393
Nyingine ni Kigustar Enterprisess, Leonardo Automotive Garage, Nedea Enterprisess, RaaR Investment, Kigoma Garage, Adam Motor na Point A.
Mkala amesema wamelazimika kumuomba Waziri Mkuu aingilie kati baada ya hatua alizozianza mwanzoni mwa mwaka huu, kuzitaka wizara na idara za serikali ambazo ndizo zilizohudumiwa na gereji hizo!kulipa madeni yao wanayodaiwa kushindwa kufanikiwa.
“Hizi Idara na wizara tulizozihudumia tunazo taarifa kwamba baada ya agizo la Waziri Mkuu wamelipa fedha lakini Meneja wa MT Depot hataki kutulipa,” amesema.
Alipotafutwa kuzungumzia madai hayo, Meneja wa MT Depot, Injinia Maronga, amesema yeye siyo msemaji wa taasisi hiyo na kumuelekeza mwandishi wa habari hizi kumtafuta Ofisa Habari ya Temesa, Theresia Mwami.
Mwami alipotafuta na kuulizwa kuhusu madai hayo, alisema hana majibu na kumtaka mwandishi awasiliane na Mtendaji Mkuu wa Temesa Dk. Stephen Masele.
Mtendaji wa Temesa alipotafutwa na kuulizwa kuhusu madeni hayo, alikiri taasisi hiyo kudaiwa lakini alitaka mwandishi apate nafasi ya kumfafanulia madeni hayo.
“Nipo Dodoma kuna vikao tunaendelea navyo, nitakupigia baadaye au njoo Dodoma,” amrsema Masele.
Hata hivyo, taarifa zilizopatikana kutoka Ofisi za Mhasibu Mkuu wa MT Depot zimedai kuwa fedha zilizokusanywa hazizidi shilingi milioni 500 ambapo Temesa wameziweka wakisubiri maelekezo ya Waziri Mkuu ili waweze kuwalipa wazabuni hao.
“Kiukweli hili suala ni dogo sana, lakini mtendaji wetu anasubiri kupata maelekezo ya nani na nani alipwe, ” alisema na kuongeza, “Temesa kama Temesa na sisi tunazidai hizo Idara na Wizara za serikali karibu Shilingi billion 5.
Wazabuni hao, wanalalamika kuwa kutolipwa madeni yao tangu 2016 kunasababisha washindwe kujiendesha kwa vile nao wanadaiwa fedha nyingi na taasisi za fedha.