NA MWANDISHI WETU
MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amesema serikali ya itajenga kituo kipya cha afya katika Kata ya Irugwa, Wilaya ya Ukerewe mkoani Mwanza ili kuwaondolea adha ya kusafiri umbali mrefu wananchi wa kata hiyo kufuata huduma za kitabibu
Akizungumza leo na wakazi wa Kata ya Irugwa wakati wa mkutano wa kumuombea kura mgombea urais wa CCM Rais John Magufuli, amesema uamuzi huo unakwenda sambamba na ahadi ya Ilani ya Uchaguzi ya 2020 – 2025.
Majaliwa amesema katika ilani ya uchaguzi ya 2020-2025, ukurasa wa 186 unasomeka, “hadi kufikia 2025 serikali itaongeza vituo vya kutolea huduma za afya kwa asimilia 20 ya vituo 8,446 vilivyopo sasa; vipaumbele vitawekwa katika ujenzi wa vituo vya afya na ukamilishwaji wa maboma kwa kuzingatia uwiano wa kijiografia, idadi ya watu na wingi wa wagonjwa.”
Amesema Serikali ya Rais Magufuli imekwishatoa sh milioni 49.2 kwa ajili ya ujenzi wa jengo moja la kujifungilia katika Zahanati Irugwa.
Akizungumza kuhusu utekelezaji wa miradi ya maji kama ilivyoainishwa kwenye ilani ya uchaguzi, alisema imeweka mipango imara ya kushughulikia upatikanaji wa maji vijijini kama hatua ya kutekeleza azma ya Rais Magufuli ya kumtua mama ndoo kichwani.
Kuhusu usafiri wa majini, Majaliwa amesema Serikali ya CCM ikiingia madarakani inakusudia kujenga vivuko mbalimbali kikiwemo kivuko cha Irugwa, Murtanga, Gana, Kakakuru na Lugezi hadi Kisorya.
“Kwa mujibu wa ilani ya uchaguzi ya CCM, ukurasa wa 83 hadi 84, Chama Cha Mapinduzi kimeielekeza serikali ikamilishe ujenzi wa vivuko vipya nane kikiwemo cha Irugwa – Murutanga wilayani Ukerewe.
“Pia ilani imeelekeza serikali ianze kutekeleza mradi wa ujenzi wa maegesho ya Lugezi – Kisorya mkoani Mwanza, Kome na Nyakalilo mkoani Mwanza, Utete huko Pwani, Chato- Nkome huko Geita, Iramba na Majita mkoani Mwanza na Irugwa,” alisema.