MAHAKAMA ya Wilaya ya Kyela mkoani Mbeya imemhukumu Brown Frank Mwaitubi (31), mkazi wa Kajunjumele, kifungo cha miaka 30 jela baada ya kupatikana na hatia ya kuwa na dawa za kulevya aina ya bangi.
Hukumu hiyo imetolewa Aprili 24, 2026 na Hakimu wa Mahakama hiyo, Rosta Mofuga, baada ya mshitakiwa kukutwa na kete 20 za bangi zenye uzito wa gramu 896.35.
Ilielezwa mahakamani hapo kuwa Mwaitubi alitenda kosa hilo Agosti 18, 2025 baada ya askari kumkuta akiwa amehifadhi dawa hizo nyumbani kwake kwa lengo la kuziuza.
Mshitakiwa alitiwa hatiani kwa mujibu wa kifungu cha 16(1) na 16(2)(c) cha Sheria ya Udhibiti na Usimamizi wa Dawa za Kulevya, Sura ya 95, Marejeo ya mwaka 2023.
Akiwasilisha hoja zake mahakamani, Mwendesha Mashitaka wa Serikali, Wakili Brice Kessi (SA), aliiomba mahakama kutoa adhabu kali kwa mujibu wa sheria ili iwe fundisho kwa mtuhumiwa pamoja na jamii.






