WASHINGTON DC, Marekani
Rais wa Marekani, Donald Trump, ameibuka na kauli kali dhidi ya kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Leo XIV, baada ya Papa huyo kukosoa msimamo wa Marekani kuhusu Iran pamoja na sera zake za uhamiaji.
Papa Leo XIV, ambaye ndiye mzaliwa wa kwanza wa Marekani kuchaguliwa kushika nafasi hiyo ya juu ndani ya Vatican, alieleza wazi kuwa vitisho vya Marekani dhidi ya Iran siyo njia sahihi ya kutatua migogoro, huku akisisitiza kuwa sera za uhamiaji zinazotekelezwa na Marekani hazikubaliki.
Kauli hiyo imeonekana kumkera Rais Trump, ambaye amejibu kwa maneno makali kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Truth Social, akimtaja Papa Leo kama “dhaifu na mhalifu.”
Katika ujumbe wake, Trump amemtaka Papa huyo kuachana na masuala ya siasa na badala yake ajikite katika jukumu lake la kiroho la kuongoza Kanisa Katoliki.
“Leo anapaswa kutekeleza majukumu yake kama Papa, atumie akili… aelekeze nguvu katika majukumu yake ili awe Papa mkubwa, siyo kuwa mwanasiasa,” ameandika Trump.
Hata hivyo, Trump hakukomea hapo, kwani alidai pia kuwa Papa Leo alichaguliwa kushika wadhifa huo kwa lengo la kuushambulia uongozi wake, akionesha kuwa mgogoro wa maneno kati yao unaendelea kuchukua sura ya kisiasa na kidiplomasia.
Imeandaliwa na Hassan Mwasha






