Kamishna wa Polisi Jamii nchini (CP) Alex Mkama, Aprili 13, 2026 amewasili mkoani Rukwa kwa ziara ya kikazi ambapo amepokelewa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Rukwa, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Shadrack Masija, akishirikiana na maafisa wengine wa Jeshi la Polisi mkoani humo.
Mara baada ya kuwasili, Kamishna Mkama alipatiwa taarifa ya hali ya usalama na ulinzi wa Mkoa wa Rukwa, iliyowasilishwa na kamanda wa Polisi wa Mkoa huo. Taarifa hiyo ilibainisha mwenendo wa matukio ya uhalifu pamoja na hatua zinazochukuliwa katika kuimarisha usalama wa wananchi na mali zao.
Aidha, Kamishna Mkama amefanya kikao kifupi cha kazi na maafisa wa Jeshi la Polisi mkoani humo, ambapo ametoa maelekezo mbalimbali ya kiutendaji yakilenga kuongeza ufanisi, nidhamu na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu ya kipolisi, hususan katika kuimarisha dhana ya Polisi Jamii.








