Serikali kupitia Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, imesitisha uchaguzi wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC) uliokuwa ufanyike Aprili 12, 2026.
Uamuzi huo umechukuliwa kufuatia malalamiko yaliyotolewa na baadhi ya wagombea, wakidai kukosekana kwa uwazi, haki na usawa katika mchakato mzima wa uchaguzi huo.
Akizungumza kuhusu hatua hiyo, Serikali imeeleza kuwa kusitishwa kwa uchaguzi ni hatua ya muda inayolenga kutoa nafasi kwa uchunguzi huru kufanyika pamoja na kurekebisha kasoro zilizojitokeza katika mchakato huo.
Aidha, imeelezwa kuwa kamati ya muda imeundwa kusimamia shughuli za TOC wakati uchunguzi ukiendelea. Kamati hiyo itashirikiana na taasisi mbalimbali ikiwemo TAKUKURU na Jeshi la Polisi ili kuhakikisha haki inatendeka na taratibu zote zinafuatwa ipasavyo.
Serikali imesisitiza dhamira yake ya kuhakikisha uchaguzi wa haki na uwazi unafanyika mara baada ya uchunguzi kukamilika.








