MKAGUZI wa Polisi wa Kata ya Picha ya Ndege, Halmashauri ya Mji Kibaha mkoani Pwani, Ibrahim Makaruti, ametoa elimu kwa wazazi kuhusu umuhimu wa malezi bora kwa watoto, akisisitiza kuwa malezi yasiyo sahihi yanaweza kuwa chanzo kikuu cha vitendo vya ukatili dhidi ya watoto.
Akizungumza na wazazi hao Aprili 10, 2026, Makaruti amesema baadhi ya wazazi wanashindwa kuwalea watoto kwa uangalizi mzuri na kuwajengea maadili mema, hali inayosababisha watoto kukua katika mazingira hatarishi na hivyo kujiingiza katika vitendo vya unyanyasaji, ukatili pamoja na makundi mabaya.
Amesisitiza umuhimu wa wazazi na walezi kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuhakikisha watoto wanalindwa na wanapatiwa uangalizi wa karibu ili kuzuia matukio ya ukatili.
Aidha, amewahimiza wazazi kuwa karibu na watoto wao kwa kusikiliza changamoto zao na kuwapatia malezi yatakayowajenga kuwa raia wema wa baadaye.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani linaendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu malezi bora ya watoto ili kudhibiti vitendo vya ukatili, ambavyo vina madhara makubwa kwa watoto na mustakabali wa taifa kwa ujumla.






