RIPOTA PANORAMA
KAMANDA wa Polisi, Mkoa wa Katavi, SACP Kaster Ngonyani amethibitisha vifo vya watu watatu wa familia moja na wengine watatu kujeruhiwa kwa ajali ya moto iliyotokea katika Kijiji cha Ilunde, Kata ya Ilunde, Wilaya ya Mlele mkoani humo.
Kamanda Kaster amesema tukio hilo lilitokea Machi 5, 2026, majira ya saa sita usiku katika Kitongoji cha Miembeni baada ya nyumba hiyo kuungua moto.
Amewataja waliofariki katika ajali hiyo kuwa ni Winfrida Sheka (32), Peter Lumilija (9) na Thabiza Lumilija (5) wote wakazi wa Kitongoji cha Miembeni.
Amewataja majeruhi watatu kuwa ni Paschal Lumilija (37), Ratifa Lumilija (7) na Elisha Lumilija (1), ambao hali zao zinaendelea vizuri wakipata Huduma ya matibabu katika kituo cha Afya Ilunde.
Kaster ameeleza chanzo cha moto huo kuwa ni mafuta ya petroli yaliyokuwa yamehifadhiwa ndani ya chumba cha kupikia.
Amesme mafuta hayo yalihifadhiwa na Paschal Lumilija ambaye hujishughulisha na biashara ya kuuza mafuta.
“Miili ya marehemu imefanyiwa uchunguzi katika Kituo cha Afya Ilunde kabla ya kukabidhiwa kwa ndugu kwa ajili ya taratibu za mazishi,” amesema Kamanda Kaster
Ametoa wito kwa wananchi kuchukua tahadhari wanapohifadhi vitu vinavyoweza kusababisha milipuko au moto majumbani, akisisitiza kuwa si salama kuhifadhi mafuta ya petroli ndani ya nyumba za kuishi bali yanapaswa kuwekwa katika maeneo maalumu ya kuuzia mafuta.
