DAR ES SALAAM
KATIBU Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Veronica Nduva ametoa shukrani za dhati kwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa ushirikiano wa karibu alioupata katika kipindi chote cha utumishi wake katika EAC.
Nduva amemtaja Rais Samia kama kiongozi mwenye uchu wa maendeleo ya jumuiya na anayethamini nafasi ya mwanamke katika uongozi.

Veronica Nduva
Aidha, amemsifu Rais Samia kwa utayari wake wa kushirikiana naye wakati wote, akisisitiza kuwa Tanzania inaendelea kutambulika kama kinara wa mtangamano na maendeleo ya jumuiya na kwamba uongozi wa Rais Samia umeongeza msukumo wa ajenda hiyo kwa maslahi ya wananchi wa Afrika Mashariki.
Vilevile, amemshukuru Rais Samia kwa ushirikiano, msaada na uwezeshaji alioupata akiwa Tanzania akibainisha kuwa muhula wake unatarajiwa kumalizika mwezi Aprili 2026.
Kwamba kwa msingi huo, ziara hiyo ilikuwa ya heshima ya kumuaga na kusisitiza thamani ya ushirikiano kati ya Tanzania kama nchi mwenyeji na Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Kwa upande wake, Rais Samia amesema Tanzania ni mdau mkubwa wa shughuli za maendeleo Afrika Mashariki na itaendelea kuunga mkono ajenda za kikanda zinazolenga kuleta maendeleo kwa wananchi, ikiwemo kurahisisha biashara kati ya nchi wanachama, kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, pamoja na masuala mengine ya kipaumbele.
Rais Samia amempongeza Nduva kwa mchango wake wa kuimarisha biashara ndani ya jumuiya na kueleza kuwa Tanzania inaendelea na marekebisho ya itifaki ya umoja wa forodha ili kuruhusu uendeshaji wa kamati ya marekebisho ya biashara (trade remedies committee) kabla ya kuiwasilisha katika ofisi ya katibu mkuu wa jumuiya hiyo.
Kadhalika, Rais Samia amesisitiza kuwa Tanzania inatambua jukumu lililo mbele ya wakuu wa nchi la kuteua katibu mkuu mpya wa EAC na kwamba Tanzania imeweka mkazo katika kupata kiongozi bora kwa kuzingatia katiba ya jumuiya na kanuni ya mzunguko (rotation) baina ya nchi wanachama.
Tanzania itaunga mkono yeyote atakayeteuliwa au kupendekezwa kuwa mwenyekiti au katibu mkuu wa jumuiya.
Mazungumzo hayo pia yalilenga kukamilisha hatua za mwisho za maandalizi ya mkutano wa wakuu wa nchi wa EAC utakaofanyika Machi 7, 2026 jijini Arusha, ambapo Rais Samia amesisitiza uongozi, utayari na dhamira ya Tanzania kuhakikisha mkutano huo unafanyika kwa mafanikio kwa kutoa ushirikiano na mazingira wezeshi yanayostahili kama nchi mwenyeji.

Rais Samia Suluhu Hassan akizungumza na Katibu Mkuu wa jumuiya ya Afrika Mashariki, Veronica Nduva.
Miongoni mwa ajenda zinazotarajiwa kujadiliwa katika mkutano huo ni uteuzi wa katibu mkuu mpya wa EAC, sambamba na masuala mengine ya kipaumbele kwa maendeleo na mtangamano wa Jumuiya
