Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Jerry Murro akikagua uzalishaji wa ‘Gypsum’ katika kiwanda cha mwekezaji mzawa kilichofunguliwa wilayani humo
MWANDISHI WA PANORAMA
Kiwanda kipya cha kutengeneza ‘Gypsum’ kinachomilikiwa na mwekezaji mzawa kimeanza uzalishaji wilayani Arumeru.
Kiwanda kicho kimefunguliwa baada ya Mkuu wa Wilaya ya Arumeru (DC), Jerry Murro kumshika mkono mwekezaji ambaye alikuwa akikabiriwa na changamoto mbalimbali, kubwa ikitajwa kuwa ni urasimu wa watendaji serikalini.
Akizungumza jana wakati wa ziara yake kiwandani hapo, DC Murro alisema anayo furaha kuona kiwanda hicho sasa kimeanza kufanya kazi huku kikitarajiwa kutoa ajira kwa watu zaidi ya 500.
DC Murro ambaye alipata wasaa wa kuzungumza na wafanyakazi kiwandani hapo, alisema awali mwekezaji wa kiwanda hicho alikuwa na changamoto ya kutokupata kibali cha ubora kutoka Shirika la Viwango (TBS) na tozo nyingi alizotakiwa kulipa wakati alikuwa bado anajipanga kuzalisha.
Alisema alipata fursa ya kuonana naye na kuanza kupangua changamoto moja baada ya nyingine mpaka alipopata kibali cha TBS na kwamba uongozi wa wilaya ulimsaidia kufunga mtambo wa kisasa ambao umeongeza uzalishaji maradufu kiwandani hapo.
![]() |
Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Jerry Murro akiwa katika ziara ya kukagua uzalishaji wa ‘Gypsum” katika kiwanda kilichofunguliwa wilayani kwake na mwekezaji mzawa |
“Nakumbuka wakati Wachina wanamfungia mtambo huu ilibidi niusimamie ili ukamilike kwa wakati maana baadhi ya watumishi wasiokuwa waaminifu walianza kumsumbua na kutaka kumkwamisha kwa sababu ya upungufu wa baadhi ya sheria na kanuni zetu.
“Leo ninafurahi kuona ndoto yangu ya kuwasaidia wananchi wenye nia ya dhati ya kuwekeza imeanza kuzaa matunda. Kiwanda hiki ni cha kisasa sana, uzalishaji wake ni kiwango cha kimataifa, kitaajiri wananchi wetu zaidi ya 500 na kina mitambo ya kisasa kabisa,” alisema DC Murro.
Alisema uchumi wa kati ambao Tanzania imefikia unahitaji viwanda vya kisasa ambavyo pamoja na kutoa ajira kwa wananchi pia vitalipa kodi serikalini.