NA DUKULE INJENI
SIMBA v/s KAIZER CHIEFS
TAIFA WANALOTOKA
Tanzania Afrika Kusini
MSIMAMO KWENYE LIGI
1 10
JINA NA UTANI
Wekundu wa Msimbazi Amakhosi
KUANZISHWA
1936 1970
NAHODHA
John Bocco Itumeleng Khune
KOCHA
Didier Gomes Gavin Hunt
MUDA – Saa 1 usiku
UWANJA – FNB
REFA: NEANT ALIOUM (CAMEROON)
MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu Bara, Simba, wanashuka Uwanja wa FNB au ukipenda Soccer City jijini Johannesburg nchini Afrika Kusini baadaye leo saa moja usiku kuwakabili wenyeji, Kaizer Chiefs mchezo wa kwanza robo fainali Ligi ya Mabingwa Afrika.
Tangu kutua jijini Johannesburg Jumanne Mei 11, Simba wamekua gumzo huku wakipewa nafasi kubwa kusonga mbele kwenye michuano hiyo mikubwa barani Afrika katika ngazi ya klabu.
Kinachoifanya Simba kuwa gumzo bondeni ni kutokana na namna ambavyo wameikabili michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu huu.
Simba inayofundishwa na Mfaransa, Didier Gomes walimaliza nafasi ya kwanza katika kundi lao lililokuwa na mabingwa watetezi Al Ahly ya Misri, AS Vita ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Al Merrikh ya Sudan.
Wekundu wa Msimbazi watakuwa wanawavaa Kaizer Chiefs wakisaka ushindi wa pili ugenini kwenye michuano hiyo baada ya kuwafunga AS Vita bao 1-0 Stade des Martyrs jijini Kinshasa katika mchezo wa kwanza Kundi A.
Nahodha wa Simba, John Bocco amekaririwa akisema hawajafuzu robo fainali kwa kubahatisha ila ni kwa kupambana na kuhakikisha wanatimiza malengo waliyojiwekea msimu ulipoanza.
“Nina imani kubwa hatukufika robo fainaki kwa bahati lakini tumefika hatua hii kwa jitihada na malengo yetu ya kuhakikisha tunafanya vizuri kwenye michuano yote,” alisema.
Bocco alisema kwa maandalizi mazuri na watu wote kushirikiana kama timu bado wanayo nafasi nzuri ya kufika mbali katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
“Tuna imani ya kupata matokeo mazuri Afrika Kusini, tunajua Kaizer Chiefs ni timu nzuri, hatuwezi kuwadharau, tunawaheshimu lakini pia tunayo malengo tuliyojiwekea kabla ya msimu kuanza na hicho ndicho kinachotusukuma kufanya vizuri.”
Licha ya Kaizer Chiefs kutinga hatua ya robo fainali Ligi ya Mabingwa Afrika, mwenendo wao Ligi Kuu Afrika Kusini sio mzuri kwani hawajaonja ladha ya ushindi katika michezo minne mfululizo.
Mashabiki tayari wameshaanza kushinikiza kocha Gavin Hunt atimuliwe kutokana na uwezekano wa timu yao kujikuta ikitakiwa kupambana kutokushuka daraja badala ya kuwania taji.
Mechi ya mwisho ya ligi ya Kaizer Chiefs ilikuwa Jumatano Mei 12 dhidi ya Moroka Swallows iliyomalizika kwa sare ya bao 1-1 na kocha Hunt alieleza kusikitika kwake kwa mechi hiyo kuchezwa siku tatu kabla ya kuwavaa Simba ambao walikuwa Afrika Kusini na kupata nafasi ya kuwaona.
“Nadhani haikua wazo nzuri sisi kucheza katikati ya wiki huku tukiwa na mchezo wa robo fainali lakini ndiyo imeshatokea,” alisema Hunt.
Kocha huyo aliongeza kusema hawawafahamu vyema Simba japo amewatazama mara chache kwenye runinga.
Kaizer Chiefs watawakosa wacheza wao muhimu, nahodha ambaye pia ni kipa Itumeleng Khune na straika Khama Billiat huku wakiwa na matumaini beki Erick Mathoho atarudi uwanjani baada ya kupata jeraha na Njabulo Blom aliyekosa mchezo dhidi ya Swallows kutokana na kutumikia adhabu.