Na Jerry Murro
MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amefanya ziara ya kukagua ujenzi wa Miundombinu ya Maji ambayo itaongeza wigo wa upatikanaji wa maji katika Jiji la Dar es Salaam.
Makonda amekagua ujenzi wa vituo vya usambazaji wa maji vinavyojengwa katika maeneo ya Changanyikeni, Makongo, Wazo na Bunju ambavyo vitasaidia kuzalisha maji ya kutosha.
Pia, mkuu huyo wa mkoa alikagua ujenzi wa visima 10 ambavyo aliahidi vitajengwa wakati wa ziara yake kuelezea kusudio la azma ya Serikali ya Mkoa wa Dar es Salaam ya kujenga Dar es Salaam mpya.
Ujenzi wa visiwa hivyo ambavyo vitahudumia wakazi wa Wilaya ya Ubungo umekamilika na kila kisima kitakuwa na uwezo wa kuzalisha lita 16,000.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, alisema lengo la Serikali ya Awamu ya Tano ni kumtua Mama ndoo ya maji kichwani na kuhakikisha huduma ya maji inawafikia wananchi wote.
Akiwa katika eneo la Jangwani ambako ujenzi wa mfumo wa maji taka unaendelea, alisema sh. bilioni 200 zinatumika katika mradi huo na mradi kama huo unaojengwa eneo la Kilongawima, Mbezi Beach unatarajiwa kutumia sh. bilioni 135, ambazo ni fedha za ufadhili zilizotolewa na Banki ya Dunia na Serikali ya Japan.
“Serikali inaendelea kufanya jitihada za kuhakikisha wakazi wa Wilaya za Kigamboni na Temeke wanapata maji ya kutosha kupitia miradi mbalimbali inayoendelea,” alisema Makonda.