![]() |
Mkurugenzi wa Wilaya ya Kinondoni, Aron Kigurumjuli |
NA MWANDISHI WETU
MKURUGENZI wa Halmashauri ya Wilaya ya Kinondoni, Aron Kigurumjuli amesema mkandarasi aliyepewa kandarasi ya kujenga soko jipya la Tandale, Namis Corporation LTD ni mwizi mdogo mdogo ambaye akikamatwa hurejesha alichoiba.
Kigurumjuli aliyasema hayo wiki iliyopita katika mahojiano maalumu na Tanzania PANORAMA Blog yaliyofanyikia Kinondoni Dar es Salaam.
Alikuwa akijibu kuhusu madai kuwa, mkandarasi huyo alighushi leseni yake ya biashara na alibainika kutenda kosa hilo wakati akisaka zabuni ya ujenzi wa soko la Tandale.
Katika majibu yake, Kigurumjuli alisema Namis Corporation LTD haikughushi leseni ya biashara isipokuwa ilifanya udanganyifu ulioiwezesha kuwa inalipa pesa kidogo kinyume na hitaji la leseni yake na hivyo ikawa inaiibia serikali pesa kidogo za tozo ya leseni.
Kigurumjuli alisema, wataalamu wake walibaini kuwepo kwa dosari hiyo kwenye leseni ya Namis Corporation LTD wakati wa ukaguzi wa nyaraka uliofanyika kabla ya kuzawadiwa zabuni ya ujenzi wa soko la Tandale.
“Unasema inadaiwa si ndiyo? sasa mimi nakwambia madai hayo ni uongo. Namis hajaghushi leseni ya biashara, sema, acha nikusaidie yule alikuwa akiiba kidogo hela za serikali. Ni mwizi mdogo mdogo tu lakini tulimbaini tukambana, akakiri tukampiga faini, akalipa.
“Alikuwa anaibaje, sikiliza. Leseni za biashara zipo za aina nyingi sana, zipo za mpaka Dola za Marekani 200,000. Huyu leseni yake alipaswa alipie kiwango cha juu lakini yeye akakataka ya kiwango cha chini, akawa analipa below ya kiwango anachopaswa kulipa. Kama sikosei kwa shughuli zake za ukandarasi alipaswa kulipa 60,000 lakini yeye akawa analipa 30,000.
” Sasa wakati wa ukaguzi wa nyaraka zake alipokuwa ameomba tenda ya soko la Tandale wataalamu wangu wakagundua huyu anatuibia, anaiibia serikali. Wakambana, alibishabisha kidogo lakini alibanwa haswa akakubali kulipa.
“Tulimpiga faini kubwa. Shilingi milioni nane ya miaka mitano aliyokuwa amefanya ujanja wake. Sasa huyu huwezi kumpa kosa kubwa hilo la kughushi, huyu ni mwizi mdogo mdogo tu na alibanwa akalipa. Hayo mengine sasa kamuilize mwenyewe,” alisema Kigurumjuli.
Tanzania PANORAMA Blog imemtafuta Mkurugenzi wa Namis Corporation LTD, Thomas Uiso kuzungumzia suala hilo bila mafanikio kwani tongu aliposema mambo yote yanayohusiana na kukwama kwa ujenzi wa soko jipya la Tandale ambalo yeye ndiye mkandarasi aulizwe Mkurugenzi Kigurumjuli amekuwa hapokei simu wala kujibu ujumbe wa maandishi.
Tanzania PANORAMA jana lilimpigia simu Uiso hakupokea na lilimtumia ujumbe wa maandishi kumuuliza kuhusu jambo hilo hakuujibu licha kuonyesha umemfikia na ameusoma.
Taarifa zilizolifikia Tanzania PANORAMA Blog zilieleza kuwa kampuni hiyo ulighushi leseni ya biashara na ilipata kandarasi mbalimbali kwa kutumia leseni hiyo ya kughushi.