NEW YORK, Marekani
UTALII ni miongoni mwa sekta muhimu zaidi duniani, ikitajwa kuchangia takribani Dola za Marekani trilioni 11.7 kwenye Pato la Dunia kwa mwaka 2025 pekee. Sekta hiyo inaendelea kuwa injini ya ajira, mapato ya Serikali, biashara za ndani na uwekezaji, hasa katika mataifa yanayopokea idadi kubwa ya wageni kutoka nje.
Hata hivyo, mchango wa utalii hutofautiana kati ya nchi na nchi. Wakati baadhi ya mataifa hutumia utalii kama sekta ya ziada, yapo ambayo uchumi wake kwa kiasi kikubwa unategemea wageni na shughuli zote zinazohusiana na safari, mapumziko na burudani.
Ripoti za Umoja wa Mataifa (UN) pamoja na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) zinaonesha orodha ya nchi ambazo utalii ni “uti wa mgongo” wa uchumi wao, kwa kuchangia sehemu kubwa ya pato la taifa.
Kulingana na takwimu hizo, Macao, eneo maalum linalopatikana Kusini mwa Pwani ya China, linaongoza duniani kwa kutegemea zaidi sekta ya utalii.
Takwimu zinaonesha kuwa mapato yatokanayo na utalii yanafikia Dola bilioni 32.4, sawa na asilimia 70.8 ya uchumi wake wenye thamani ya Dola bilioni 45.8.
Nafasi ya pili inashikiliwa na Aruba, kisiwa kinachohusishwa na Uholanzi, ambacho uchumi wake unategemea utalii kwa asilimia 69.7.
Nchi nyingine zinazofuata kwa utegemezi mkubwa wa utalii ni:
- Maldives kwa asilimia 68.1
- Andorra kwa asilimia 66.5
- Saint Lucia kwa asilimia 53.8
Kwa upande wa Bara la Afrika, Visiwa vya Ushelisheli (Seychelles) vinaongoza kwa utegemezi mkubwa wa utalii, ambapo sekta hiyo inachangia asilimia 46.6 ya uchumi wake.
Takwimu hizi zinaonesha wazi kuwa utalii si tu sekta ya burudani, bali ni mhimili mkubwa wa uchumi wa mataifa mengi duniani, hususan visiwa na nchi ndogo zinazotegemea zaidi mapato ya wageni wa kimataifa.






