MAKONDA NA “KOFIA YA UNABII” SEKTA YA MICHEZO

Date:

Share post:

WAUMINI wa dini mbili kubwa nchini, Uislam na Ukristo, wanaweza kukubaliana kwa urahisi kwamba manabii (mitume) walitumwa katika jamii zilizokuwa zimezama kwenye maovu na kupoteza mwelekeo wa maisha. Kusudio lao halikuwa tu kuhimiza ibada sahihi, bali kurekebisha mwenendo wa jamii kwa ujumla, kuijenga kimaadili, kiuchumi na kijamii.

Katika simulizi za Qur’an na Biblia, tunakumbushwa mfano wa Nabii Musa ambaye alikuta jamii ya Wamisri ikiwa imeoza: kuabudu sanamu, kushamiri kwa ushirikina, ulevi na hata kamari. Kwa ufupi, dhamira ya Mungu kwake ilikuwa ni kuibadili jamii hiyo na kuirejesha katika njia iliyo sahihi na yenye manufaa.

Taswira hiyo ndiyo inanifanya nimtazame Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Paul Makonda, katika nafasi yake ya sasa. Na hapa ninamaanisha kwa uzito wote: ameingia kwenye sekta yenye changamoto nyingi, inayohitaji “mtu wa mabadiliko.”

Ukweli usiohitaji mjadala mrefu ni kwamba sekta ya michezo imekuwa mhimili muhimu wa maendeleo nchini. Mbali na kodi zinazolipwa na klabu, vyama na mashirikisho, michezo pia imekuwa ikipunguza mzigo wa ajira kwa Serikali kwa kutoa fursa kwa vijana wengi kujiajiri na kuajiriwa.

Zaidi ya hapo, michezo imekuwa na mchango mkubwa katika kuinua sekta nyingine, hususan utalii. Kupitia mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho, klabu kutoka mataifa mbalimbali zimekuwa zikija nchini na kuleta “ulaji” kwa hoteli, usafiri na biashara za ndani.

Na sasa, Tanzania ikijiandaa kuwa mwenyeji wa fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) kwa kushirikiana na majirani Kenya na Uganda, hakuna shaka kuwa utalii na uchumi kwa ujumla vinatarajiwa kufaidika zaidi.

Hata hivyo, pamoja na faida zote hizo, sekta ya michezo imeendelea kubeba mzigo mkubwa wa migogoro, inayochangiwa zaidi na udhaifu wa uongozi. Kwa miaka mingi, migogoro imekuwa kama sehemu ya maisha ya kawaida ndani ya vyama na mashirikisho.

Vyanzo vyake vimekuwa vikijirudia: viongozi kung’ang’ania madaraka, “figisu” za uchaguzi, ukosefu wa uwazi wa mapato na matumizi, pamoja na malalamiko ya mifumo kandamizi isiyotoa haki kwa wanachama na wadau.

Kwa mazingira hayo, ni wazi kabisa Waziri Makonda amepewa wizara yenye “moto”—sekta yenye hitaji kubwa la kusafishwa na kurekebishwa, kama ambavyo manabii walitumwa kwenye jamii zilizojaa uovu.

Lakini kwa bahati nzuri, hatua chache alizochukua tangu ateuliwe zimeanza kuibua matumaini mapya na kurejesha tabasamu kwa wadau wa michezo waliokuwa wameanza kukata tamaa.

Katika mkutano wake na Baraza la Michezo la Taifa (BMT) pamoja na viongozi wa vyama na mashirikisho uliofanyika Machi 13, 2026, Waziri Makonda aligusa maeneo nyeti kwa ujasiri, akionyesha uelewa mpana wa matatizo yaliyopo na kuweka wazi njia anazotaka kuzitumia kuyatatua.

Alisema: “Viongozi wote wa vyama na mashirikisho ya michezo ambao hawajatekeleza ahadi walizotoa wakati wa kuomba uongozi nitawafuatilia. Nikibaini kuwa uongozi haujafikia hata asilimia 20 ya malengo, nitawaondoa bila huruma, kwa kuwa nafasi hizo zimepatikana kwa kura za wanachama.”

Kauli hii inaonyesha dhamira ya kuijenga sekta ya michezo katika msingi wa uwajibikaji—utamaduni ambao kwa muda mrefu umekuwa ukikosekana kwa baadhi ya viongozi.

Hatua yake nyingine iliyoibua gumzo kubwa ni uamuzi wa kuusimamisha uchaguzi wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), kufuatia malalamiko ya baadhi ya wagombea. Hili limeonekana kama ishara ya wazi kuwa hataki kuona michakato ya uchaguzi inachafuliwa na mizengwe, upendeleo au mifumo isiyo na usawa.

Kwa ujumla, jitihada za Waziri Makonda zinapaswa kuangaliwa kwa jicho chanya. Lengo lake linaonekana kuwa ni kuondoa mfumo wa “bora liende” ambao kwa miaka mingi umeikwamisha michezo ya Tanzania, kuua vipaji na kuifanya sekta yenye nafasi kubwa ibaki kuwa ya migogoro badala ya maendeleo.

Na kama kweli atasimamia alichokisema kwa vitendo, basi si ajabu kusema: huenda Waziri Makonda ameivaa “kofia ya unabii” katika sekta ya michezo—kofia ya mtu aliyeingia kusafisha, kusahihisha na kuanzisha enzi mpya ya uwajibikaji na uwazi.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

spot_img

Related articles

SOMA HIYO! ISRAEL NDIYO WAASISI WA MIKWAJU YA PENALTI

LONDON, Uingereza NI jioni ya Agosti 5, 1970 kwenye Uwanja wa Boothferry Park mjini Hull, Manchester United ikiwa ugenini...

AMEJIPATA! LAMPARD ALIVYOREJEA EPL AKIWEKA REKODI

LONDON, Uingereza IKIWA ni miezi 18 tu imepita tangu alipoajiriwa, Frank Lampard ameiwezesha Coventry City kupanda daraja na kurejea...

USICHUKULIE POA! PATORANKING ALIUZA SUMU YA PANYA MITAANI KABLA YA ‘KUTOBOA’

LAGOS, Nigeria WAHENGA walisema maisha ni safari yenye milima na mabonde. Kwamba katika kuishi kwako, si nyakati zote zitakuwa...

KIFO CHA BOSI KINAVYOITESA LEICESTER CITY

LONDON, UingerezaMIAKA 10 iliyopita, Leicester City waliishangaza dunia walipotwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya England (EPL) mbele ya...