Kamati ya Usalama ya Mkoa wa Pwani imeanza rasmi ukaguzi wa miradi inayotarajiwa kuzinduliwa na kutembelewa na Mwenge wa Uhuru mwaka 2026, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya mapokezi ya mbio hizo muhimu kitaifa.
Ukaguzi huo ulioanza Aprili 10, 2026, unahusisha miradi mbalimbali katika halmashauri zote za Mkoa wa Pwani. Lengo kuu ni kuhakikisha miradi yote ipo katika hali nzuri na iko tayari kwa ajili ya uzinduzi wakati wa mbio za Mwenge wa Uhuru.
Kwa mujibu wa ratiba, Mwenge wa Uhuru unatarajiwa kuwasili mkoani Pwani Aprili 18, 2026, ukitokea Mkoa wa Dar es Salaam. Utapokelewa rasmi katika Wilaya ya Bagamoyo, ambako utakagua na kuzindua miradi mbalimbali ya maendeleo inayolenga kuboresha huduma kwa wananchi.
Aidha, Aprili 27, 2026, Mwenge wa Uhuru utakabidhiwa Mkoa wa Lindi baada ya kukamilisha ziara yake katika Mkoa wa Pwani.









