ACCRA, Ghana
NYOTA wa kabumbu mwenye umri wa miaka 20 nchini Ghana ameuawa baada ya watu wasiojulikana kuvamia na kulishambulia kwa risasi basi la timu yake.
Winga huyo wa klabu maarufu ya Berekum Chelsea, Dominic Frimpong, amefariki baada ya kupigwa risasi ya kichwa katika tukio hilo.
Vyanzo vya habari vinaeleza kuwa basi la wachezaji hao lilikuwa njiani kuelekea kwa wapinzani wao wa mechi ijayo, FC Samartex.
Wakiwa Barabara ya Bibiani-Goaso, watu walioshika bunduki walivamia basi lao na kuanza kumimina risasi.
Baadhi ya wachezaji na viongozi walitorokea porini ili kunusuru maisha yao na wapo ambao hawajulikani walipo hadi sasa.
Frimpong amekuwa na kiwango bora msimu huu, akifunga mabao mawili katika mechi 11.
Imeandaliwa na Hassan Mwacha






