AJI Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Arusha, Frank Habibu Mahimbali, amezindua majengo matatu ya Mahakama za Mwanzo na kurasimisha kuanza kwa shughuli za utoaji haki katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Arusha.
Mahakama hizo zimejengwa katika wilaya za Longido (Kata ya Kitumbeine), Arusha (Kata ya Terati) na Monduli, huku hafla ya uzinduzi ikifanyika katika Mahakama ya Mwanzo ya Makuyuni, wilayani Monduli.
Akizungumza katika uzinduzi huo, Jaji Mahimbali amesema hatua hiyo ni matokeo ya dhamira ya dhati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati na kwa gharama nafuu bila ubaguzi.
“Ufunguzi wa mahakama hizi ni utekelezaji wa azma ya serikali ya kusogeza huduma za haki karibu zaidi na wananchi,” amesema Jaji Mahimbali.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Monduli, . Gloriana Kimath,amesisitiza umuhimu wa watumishi wa mahakama kufanya kazi kwa weledi, uadilifu na kuepuka vitendo vya rushwa.















