![]() |
Spika wa Bunge, Job Ndugai |
NA MWANDISHI WETU
KAMATI za kudumu za Bunge zinaanza vikao vyake leo jijini Dodoma kutekeleza majukumu ya kibunge kabla ya kuanza kwa mkutano wa pili wa Bunge la 12, Februari 2, 2021.
Kwa mujibu wa ratiba ya shughuli za kamati iliyotolewa wiki iliyopita na kitengo cha mawasiliano na uhusiano wa kimataifa cha Bunge, shughuli ya kwanza itakayofanywa na kamati zote ni kuchagua wenyeviti na makamu wenyeviti wa kamati.
Baada ya kupatikana kwa viongozi wa kamati, wabunge wataanza kupewa mafunzo kuhusu taratibu za uendeshaji wa kila kamati ambayo yatafuatiwa na mafunzo kuhusu Bunge mtandao na usalama wa mtandao kwa kamati zote.
Ratiba inaonyesha kuwa shughuli nyingine itakayofanyika ni kamati za kisekta kupokea maelezo ya wizara kuhusu muundo, majukumu ya taasisi, sera na sheria zinazosimamiwa na wizara hizo.
“Mafunzo kwa Kamati za Hesabu za Serikali (PAC) Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) Kamati ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma (PIC) na Kamati ya Bajeti kuhusu uchambuzi wa taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Msajili wa Hazina (TR) na namna bora ya kuhoji maafisa masuhuli.
“Mafunzo kwa kamati ya sheria ndogo kuhusu uchambuzi wa sheria ndogo na uzoefu wa mabunge mengine ya nchi zinazofuata mfumo wa kibunge wa Jumuiya ya Madola,” inasomeka ratiba hiyo.
Kuhusu shughuli zitakazofanywa na kamati ya bajeti, ratiba hiyo inaonyesha kamari ya bajeti itapokea na kujadili taarifa ya tathimini ya utekelezaji wa mpango wa pili wa maendeleo ya taifa kwa miaka mitano 2016/17 – 2020/21.
Inaonyesha zaidi kuwa kamati hiyo itapokea na kujadili mapendekezo ya mpango wa maendeleo ya taifa wa miaka mitano 2021/22-2025/26 na mapendekezo ya mpango wa maendeleo ya taifa wa mwaka mmoja 2021/21.
Shughuli nyingine zilizomo kwenye ratiba hiyo ni kamati ya bajeti kupokea na kujadili mwongozo wa kuandaa mpango na bajeti ya serikali kwa mwaka wa fedha 2021/22 pamoja na kupokea na kujadili taarifa ya utekelezaji wa bajeti ya serikali pamoja na sheria ya fedha kwa kipindi cha nusu mwaka kwa mwaka wa fedha 2020/2021.