WAKO WAPI MAKACHERO WA KESI YA UNGA YA HARIRI NA MUNA

0
235

CHARLES MULLINDA

SERIKALI imeshindwa. Imeshindwa kesi mahakamani. Imeshindwa na mfanyabiashara Mohamedi Hariri na mkewe Muna Said, waliokuwa wakishtakiwa kwa kosa la kukutwa na dawa za kulevya aina ya Heroin Hyrochloride zenye uzito wa gram 214.11 ambazo huku kwetu uchokonozini, zinafahamika zaidi kwa jina la unga.

Mahakama Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi iliwaachia Hariri na Muna kwa kile ilichoeleza kuwa upande wa mashtaka ulishindwa kuthibitisha mashtaka bila kuacha shaka yoyote.

Mchokonozi hana tatizo na hukumu. Kazi ya mahakama ni kutenda haki bila kuangalia sura ya mtu, imetekeleza wajibu wake.

Lakini, wakati Hariri na mkewe Muna wakichekelea kuibwaga serikali, ninawaita makachero waliowatia nguvuni wawili hao kisha wakachunguza tuhuma zao kabla ya kuandaliwa kwa mashtaka kwani wana maswali kadhaa ya kujibu.

Wanapaswa kuyajibu haraka kwa sababu ni maswali mepesi na tangu kuachiwa kwa Hariri na Muna, kumekuwa na mijadala ya chini kwa chini isiyokoma ambayo hakuna shaka yoyote kuwa itakoma iwapo maswali hayo yatajibiwa.

Na kabla ya kuibuka kwa maswali hayo, makachero wetu watambue kuwa walipaswa kuanza kuandaa majibu ya maswali mepesi yaliyokuwa yakijitokeza kwa kadri kesi hiyo ilivyokuwa ikiendelea kusikilizwa mbele ya Jaji  Immaculate Banzi wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi.

Makachero wetu, katika msako wao wa Machi 2, 2018 uliowafikisha Kinondoni, nyumbani kwa Hariri na Muna walikofanya upekuzi na kuibuka na walichodai mahakamani kuwa ni unga, walipaswa kuandaa mazingira rafiki kwao ya kuhakikisha wanakuwa na ushahidi ulioshiba wa tukio zima ambao ungesaidia kuondoa sintofahamu ya aina yoyote kutoka kwa mashahidi wakati wakitoa ushahidi wao mahakamani.

Aidha, kwa akili za kichokonozi, makachero wetu walipaswa kuwaweka katika dira zao mashahidi wote wa kesi hiyo wakianza na wale wa jamhuri na wengine wote kwa sababu wachokonozi wana amini pasipo shaka kuwa kesi za aina hii, hutokea wakati mashahidi wakafanya yao kwa sababu zao wenyewe.

Mfanyabiashara Mohamedi Hariri ambaye ameshinda kesi ya kukutwa na dawa za kulevya

 

Wachokonozi tunaamini kuwa iwapo makachero wetu wangezingatia kuwaweka katika dira zao mashahidi wote wa kesi hiyo, nadhani wakati kesi inaendelea mahakamani wangefungua kesi nyingine dhidi ya baadhi ya mashahidi ambao labda kwa makusudi tu waliamua kuchezea ushahidi kwa sababu zao binafsi au kwa kushawishiwa na bila shaka wangekuwa na ushahidi usiokuwa na chembe ya shaka ambao wangeuwasilisha mahakamani kuthibitisha tuhuma dhidi ya watuhumiwa.

Kama wangezingatia haya, maswali yanayoulizwa sasa kuwa inawezekanaje askari aliyeshiriki katika ukamataji ajichanganye kutoa ushahidi mahakamani yasingekuwepo au yangekuwa yameishapata majibu kwa sababu wangekuwa na vielelezo vya kuthibitisha ushahidi wa shahidi mahakamani.

Tena, kusingekuwa na maswali tasa dhidi ya mjumbe ambaye wakati wa upekuzi alikuwa eneo la tukio akishuhudia mwenendo mzima  wa tukio la upekuzi lakini kufika mahakamani, ushahidi wake ukatofautiana na mashahidi wengine aliokuwa nao eneo la tukio?

Si nia ya Mchokonozi kuanza kuchokonoa mwenendo wa kesi hii. Hapana. Wajibu wa mchokonozi ni kuwafikirisha waliochoka au kuzembea kufikiri sawasawa, kuburudisha, kuelimisha, kuonya na kuibua yaliyofichika.

Katika kutekeleza wajibu huo, hapa narudia  kuwaalika makachero waliokuwa wakishughulika na sakata hili zito wawaeleze wachokonozi iwapo baada ya kukamatwa kwa Hariri na kutupwa msambweni, rada zao zilikuwa zikinasa nyendo za mkewe Muna ambaye alibaki uraiani akipambana kumtoa mumewe msambweni?

Walijua kuwa Muna alikuwa akikutana na nani? Nani alikuwa naye bega kwa bega katika kumpambania mumewe? Ni watu wa aina gani aliokuwa akikutana nao! hadharani na faragha? Je, walichunguza na kujua vema historia za watu hao na kutunza kumbukumbu za matukio ya kukutana kwao?

Aidha, baada ya Muna kukamatwa ni nani aliyebaki uraiani akimpambania? Alikuwa akimpambania kwa mbinu zipi? Alikuwa na maslahi gani hasa mpaka ajiingize kwenye kumpigania kwa mbinu za aina yoyote ile?

Mtu huyo. aliwafikia nani na nani kumsaidia katika mapambano hayo ya kumnasua Muna? Muna akiwa msambweni alikuwa na mawasiliano na mtu huyo? Mawasiliano hayo yalikuwa ya aina gani? Alitumia nguvu kiasi gani (kama ipo) kuhakikisha anamuokoa Muna? Historia ya mpambanaji huyo wa Muna ikoje?

Maswali haya yanapojibiwa na makachero wetu wanapaswa kujua kuwa serikali kushindwa kesi mahakamani ni fedheha. Tena inashindwa kesi ikiwa na ushahidi ulioaminika kutokuwa na lepe la shaka. Wajibu wakijua kuwa wao ni wapiganaji wa serikali iliyoshindwa mahakamani ambayo inapigana kufa na kupona kutokomeza dawa za kulevya.

Kama maswali haya machache yatajibiwa kwa ufasaha, yatazaa maswali mengine machache muhimu ambayo nitayauliza katika andiko fikirishi lijalo yatakayotuoongoza kwenda hatua nyingine ya kufikiri zaidi.

Tutafikiri kwa pamoja mrorongo wa mbinu zinazoweza kusababisha serikali kubwagwa katika kesi za aina hii.

 

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here