SHIRIKISHO la Soka Duniani (FIFA) limetangaza majina ya waamuzi sita kutoka Afrika watakaochezesha fainali za Kombe la Dunia 2026, zitakazoanza Juni 11 katika nchi za Marekani, Mexico na Canada.
Ni nafasi kubwa kwa Afrika kuendelea kuonyesha uwezo wake katika usimamizi wa soka la kimataifa na hapa ni waamuzi hao:

1. OMAR ABDULKADIR ARTAN (Somalia)
Artan, alishinda tuzo ya Mwamuzi Bora Afrika mwaka 2025, anaandika historia kwa kuwa Msomali wa kwanza kuchezesha Kombe la Dunia.
Amezaliwa Mogadishu mwaka 1992 na kupata beji ya FIFA mwaka 2018. Ana uzoefu mkubwa akiendesha mechi za Ligi ya Mabingwa Afrika, AFCON pamoja na Kombe la Dunia la U-20.
2. DAHANE BEIDA (Mauritania)
Beida anajulikana kwa kuchezesha fainali ya AFCON 2023 kati ya Ivory Coast na Nigeria.
Amehudhuria pia michezo ya Olimpiki (2020 na 2024), na mwaka 2025 alichezesha mechi ya vilabu kati ya Real Madrid na RB Salzburg katika Kombe la Dunia la Klabu.


3. MUSTAPHA GHORBAL (Algeria)
Ni miongoni mwa waamuzi wenye uzoefu mkubwa Afrika. Amekuwa mwamuzi wa FIFA tangu 2014 na mwaka 2025 alichezesha nusu fainali ya Kombe la Dunia la Klabu kati ya PSG na Real Madrid.
4. AMIN MOHAMED (Misri)
Amin Mohamed amekuwa mwamuzi wa FIFA tangu 2017, akianza kuchezesha Ligi Kuu ya Misri mwaka 2013.
Mwaka 2019 aliteuliwa kuchezesha fainali za Kombe la Dunia la U-17 zilizofanyika Brazil.


5. ABONGILE TOM (Afrika Kusini)
Mzaliwa wa Septemba 16, 1991, Tom ni mwamuzi wa FIFA tangu 2020. Amechezesha michuano mikubwa ikiwemo CHAN 2022, Ligi ya Mabingwa Afrika, Kombe la Dunia la U-20 (2023) na AFCON 2025.
6. PIERRE ATCHO (Gabon)
Licha ya kuwa na umri wa miaka 33, Atcho tayari ana uzoefu mkubwa katika ngazi ya kimataifa.Amechezesha AFCON 2025 pamoja na Kombe la Dunia la U-17.







