![]() |
Hayati Rais Dk. John Magufuli |
NA CHARLES MULLINDA
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzaniam, Dk. John Pombe Magufuli amefariki dunia katika Hospitali ya Mzena, iliyopo jijini Dar es Salaam alikokuwa amelazwa akipatiwa matibabu.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amelitangazia taifa, leo Machi 17, 2021 majira ya saa tano usiku kuwa Rais Dk. Magufuli amefariki kutokana na maradhi ya moyo.
Akizungumza na Taifa kutokea mkoani Tanga, Makamu wa Rais Samia amesema Rais Dk. Magufuli amefariki dunia majira ya saa 12 jioni baada ya kulazwa katika hospitali hiyo tangu Machi 14, mwaka huu.
Makamu wa Rais Samia amesema awali Rais Dk. Magufuli alifikishwa katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) Machi 6, mwaka huu akisumbuliwa na tatizo la moyo la mfumo wa umeme ambalo amekuwa nalo kwa zaidi ya miaka 10.
“Machi 14 mwaka huu, alijisikia vibaya akakimbizwa Hospitali ya Mzena ambako aliendelea na matibabu chini ya uangalizi wa madaktari na wauguzi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete hadi umauti ulipomkuta,” amesema Makamu wa Rais Samia.
Amesema Tanzania itakuwa katika kipindi cha maombolezo ya siku 14 na bendera zitapepea nusu mlingoti.
Aidha Makamu wa Rais Samia, amesema wananchi watajulishwa juu ya taratibu za mazishi za Rais Dk. Magufuli.