SIMBA wameambulia patupu, baada ya kiungo wa mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara Yanga, Yahaya Mudathir, kusaini mkataba wa miaka miwili wa kuendelea kuichezea timu yake ya Mtaa wa Twiga na Jangwani, jijini Dar es Salaam.
Mudathir ambaye mkataba wake ulimalizika msimu uliopita, imeelezwa amekubali kubaki Yanga, baada ya kusaini mkataba wenye thamani ya Sh. milioni 100, huku akilipwa mshahara wa Sh. milioni 13, kila mwezi, badala ya Sh. milioni 10 iliyokuwa ofa ya klabu hiyo.
Awali, kiungo huyo alikuwa anahitaji apewe Sh. milioni 150 na mshahara wa Sh. milioni 15 ili aongeze mkataba mwingine, lakini amekubali kulipwa kiasi hicho
Kabla ya kusaini mkataba huo, ilielezwa kwamba, watani wao wa jadi Simba walikuwa tayari kumpa kiasi cha fedha alichohitaji kiungo huyo ili waweze kumjumuisha katika kikosi chao cha msimu ujao.
Hivi karibuni Rais wa Klabu ya Yanga, Hersi Said, alithibitisha kuwa Simba walikuwa na mpango wa kumsajili kiungo wao, lakini ataendelea kubaki Jangwani kwa misimu miwili ijayo.