RIPOTA PANORAMA
VYOMBO vya Ulinzi na Usalama vya Tanzania ni vitiifu kwa Dola na vimefanikiwa kudhibiti kwa kiwango cha juu hali ya amani na mipaka ya nchi.
Hayo yameelezwa jana na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Alexander Makulilo alipokuwa akiwasilisha mada kuhusu hali ya siasa nchini kuelekea uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika mwakani na uchaguzi mkuu wa 2025.
Profesa Makulilo aliwasilisha mada katika mkutano maalumu wa Baraza la Vyama vya Siasa uliowashirikisha wadau wa demokrasia ya vyama vingi vya siasa kutathmini utekelezaji wa mapendekezo ya Kikosi Kazi kilichoundwa na Rais Samia Suluhu Hassan kufanyia kazi masuala yanayohusu demokrasia.
Akiwasilisha mada yake hiyo kwenye mkutano unaofanyika kwa siku tatu katika ukumbi wa mikutano wa kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam, Profesa Makulilo alisema utafiti uliofanywa mwaka 2022 na Bertelsmann Stiftung’s Transformation Index (BTI) unaonyesha kuwa hakuna kikundi chochote cha kijamii au cha kijeshi kilichopata kutoa upinzani dhidi ya vyombo vya ulinzi na usalama.
Profesa Makulilo alisema utafiti huo unaonyesha kuwa nchi haijawahi kuwa na vita au machafuko ya kisiasa ambayo yamevuruga umoja wa kitaifa na amani na Tanzania imekuwa ikijulikana duniani kama kisiwa cha amani tangu ipate uhuru, mwaka 1961.

Wajumbe wa mkutano maalumu wa Baraza la Vyama vya Siasa na wadau wa demokrasia ya vyama vingi vya siasa wakifuatilia mada kuhusu hali ya siasa nchini, iliyowasilishwa jana na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Alexander Makulilo katika ukumbi wa mikutano wa kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC.)
Aidha, Profesa Makulilo alisema utafiti uliofanywa na Global Peace Index mwaka 2021 unaonyesha Tanzania imeendelea kuwa ya amani, akishkka nafasi ya kwanza kwa nchi za Afrika Mashariki na kwa Afrika iko nafasi ya saba na ya 58 kati ya nchi 163 duniani.
“Hadi sasa, tafiti mbalimbali zinaonyesha kuwa, kwa kiasi kikubwa Tanzania imeendelea kuwa nchi ya amani duniani. Mfano: Global Peace Index (2021) inaonyesha Tanzania ilishika nafasi ya kwanza kwa amani katika nchi za Afrika Mashariki; ya saba katika Bara la Afrika na ya 58 kati ya nchi 163 duniani,” alisema Profesa Makulilo.