TERESEA MHAGAMA
Dodoma
NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Dotto Biteko jana alitoa amri nane kwa wizara mbili, Ofisi ya Rais Utumishi na wakurugenzi wa halmashauri nchini.
Amri hizo alizitoa Jijini Dodoma wakati wa hotuba yake ya ufunguzi wa mkutano wa mwaka wa kiutendaji wa maafisa Ustawi wa Jamii wa wizara za kisekta, taasisi za umma na sekta binafsi zinazotoa huduma za ustawi wa jamii nchini
Wazira zilizolengwa na amri za Dk. Biteko ni ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu na Wizara ya Afya. Pamoja na hizo ni Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na wakurugenzi wa halmashauri zote nchini.
Amri za Dk. Biteko zinalenga kuzifanya wizara, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na halmashauri nchini kuwa imara na kutoa huduma bora watu.
Katika hotuba yake hiyo, Dk. Biteko alianza na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na wadau wengine kwa kuwataka wahakikishe mchakato wa mapitio ya sheria ya mtoto na kanuni zake unakamilika ili watoto wanapate ulinzi na malezi stahiki.
Pia alielekeza mchakato wa sheria ya wataalamu wa Ustawi wa Jamii kukamilike ili kupanua wigo na kusimamia maadili ya utoaji wa huduma za ustawi wa jamii.
Kisha aliwageukia wakurugenzi wa halmashauri nchini na kuwataka kutenga fedha kwa ajili ya huduma za Ustawi wa Jamii kwa mujibu wa mwongozo wa mipango, bajeti na taarifa za Ustawi wa Jamii.
Dk. Biteko alitoa agizo mahususi kwa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma kuendelea kutoa ajira kwa maafisa Ustawi wa Jamii.
Kwa upande wa tatizo la afya ya akili, Dk. Biteko aliagiza kuimarishwa kwa programu ya huduma ya afya ya akili na msaada wa kisaikolojia ili kupunguza athari na changamoto zinazotokea ndani ya familia na jamii.
Amri nyingine aliyoitoa ni kuwekwa mfumo madhubuti wa ufuatiliaji wa makao ya watoto na makazi ya wazee ili malengo ya msingi ya kuanzishwa kwa vituo hivyo yafuatwe kikamilifu.
Aidha, aliigiza Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu kwa kushirikiana na wizara za kisekta na wadau wa maendeleo kufanya utafiti ili kupata taarifa sahihi na takwimu zitakazoboresha huduma za Ustawi wa Jamii.
Katika maagizo hayo, limo pia lililoelekezwa Wizara ya Afya moja kwa moja la kuunda kitengo maalumu cha kushughulikia uratibu wa huduma za Ustawi wa Jamii.
Alisema Serikali inaendelea kuipa kipaumbele sekta hiyo kwa kuwa imekuwa kimbilio la wananchi wenye uhitaji wa huduma inazotoa na alitoa uhakikisho wa ushirikiano kwa wataalamu wake muda wowote.
Dk. Biteko alisema Sekta ya Ustawi wa Jamii ikifanya kazi kwa weledi na ufanisi, itapunguza mzigo kwa Serikali kwa kuwa changamoto za kijamii zitapungua na fedha ambazo zimetengwa zitatumika katika kuendeleza maendeleo mengine.
Naye Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Dk. Dorothy Gwajima aliwataka watumishi wa wizara anayoiongoza kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili huduma ya Ustawi wa Jamii iwafikie wananchi wote.
Ufunguzi wa mkutano huo ulihudhuriwa pia na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Deogratius Ndejembi naNaibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu), Patrobas Katambi.