NAIBU Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir, amezindua mtaala mpya wa mafunzo ya ufundi wa aluminium na ufungaji wa vioo (Aluminium and Glass Fitting with Metal Fabrication), akieleza kuwa elimu ya ufundi inayojikita katika ujuzi wa vitendo ni njia muhimu ya kutatua changamoto ya ajira kwa vijana nchini.
Uzinduzi huo umefanyika Aprili 23,2026, jijini Dar es Salaam kupitia ushirikiano kati ya Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi VETA na Aluminium Emirates Profile.
Akizungumza katika hafla hiyo, Wanu amesema hatua hiyo inaendana na dhamira ya Serikali ya kuimarisha elimu yenye kuzingatia ujuzi ili kuzalisha wahitimu wenye uwezo wa kujiajiri na kuajiriwa kwa ufanisi.
Amesema mtaala huo umeandaliwa kwa kuzingatia mahitaji ya soko la ajira na mabadiliko ya teknolojia, huku ukiweka mkazo mkubwa kwenye mafunzo ya vitendo ili kuwajengea vijana uwezo wa kufanya kazi kwa ushindani.
“Tunataka vijana wetu wapate ujuzi unaokwenda sambamba na mahitaji ya soko la sasa na teknolojia mpya,” amesema Wanu.
Ameongeza kuwa Serikali imeelekeza kuanzishwa kwa mitaala ya aluminium katika vyuo vya VETA ili kurasimisha na kutambua rasmi ujuzi wa mafundi hao nchini.
Ameagiza VETA kuangalia uwezekano wa kuanzisha Vituo vya Umahiri kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, ili vijana waweze kupata mafunzo ya kisasa yanayohitajika zaidi kwenye soko la ajira.
Katika kuhamasisha ushiriki wa vijana, alisema atadhamini vijana 10 kutoka jimbo lake kujiunga na mafunzo hayo, huku akitoa kipaumbele kwa watoto wa kike.
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Husseni Omar, amesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za mafunzo na sekta ya viwanda ili kuhakikisha wahitimu wanapata ujuzi unaohitajika moja kwa moja katika maeneo ya kazi.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Anthony Kasore, amesema ushiriki wa mamlaka hiyo katika mpango huo ni sehemu ya mkakati wa kuhakikisha mafunzo yanayotolewa yanakidhi mahitaji halisi ya soko la ajira la sasa.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Aluminium Emirates Profile, Degratius Marandu, amesema kupitia ushirikiano huo wakufunzi na mafundi watanufaika na maarifa pamoja na teknolojia za kisasa zitakazosaidia kuongeza ufanisi na ubora katika sekta ya ujenzi nchini.












