WANANCHI wa vitongoji 15 katika Jimbo la Namtumbo, mkoani Ruvuma, wameanza kunufaika na huduma ya umeme baada ya kukamilika kwa mradi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA).
Uzinduzi wa huduma hiyo umefanywa na Mbunge wa Jimbo hilo ambaye pia ni Waziri wa Katiba na Sheria,Dk. Juma Homera, katika vitongoji vya Mtonya na Mandepwende, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita kusogeza huduma ya nishati kwa wananchi wa vijijini.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dk. Homera amesema serikali imejipanga kuhakikisha vitongoji vyote vinaunganishwa na umeme ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi.
“Mpango huu unahusisha kuunganisha vitongoji vipya kila mwezi, huku akisisitiza kuwa huduma hiyo itawafikia wananchi wote bila kujali aina ya makazi yao,”amesema Dk Homera
“Lengo la serikali ni kuhakikisha hata nyumba za nyasi zinapata umeme, ili kuboresha maisha ya wananchi na kuongeza fursa za kiuchumi,” amesema Dkt. Homera.
Kwa upande wake, mwakilishi wa REA Deo Nangu, amesema mradi huo umegharimu takribani shilingi bilioni 1.6 hadi kukamilika kwake.






