Viongozi wa jamii kutoka wilaya za Longido na Ngorongoro wamekutana na Wizara ya Maliasili na Utalii jijini Dodoma kwa lengo la kuimarisha uelewa wa pamoja kuhusu uhifadhi endelevu wa rasilimali za asili na namna unavyoweza kuongeza mchango wa sekta ya utalii katika maendeleo ya taifa.
Akizungumza katika kikao hicho, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, alisema kuwa utunzaji wa maliasili ni mhimili muhimu wa ukuaji wa sekta ya utalii, akisisitiza kuwa utalii ni miongoni mwa sekta zinazochangia kwa kiwango kikubwa mapato ya taifa na kuendelea kuwa chanzo kikuu cha ajira kwa Watanzania wengi.
Dkt. Kijaji alieleza kuwa fedha zinazopatikana kupitia utalii zimekuwa zikiwezesha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa barabara, huduma za afya, elimu, maji safi na miradi ya kijamii katika maeneo mengi nchini.
Aidha, alibainisha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mkazo katika kuhakikisha uhifadhi wa mazingira unaendana sambamba na maendeleo ya kiuchumi, huku akitoa wito kwa jamii zinazoishi maeneo ya hifadhi kuwa sehemu ya ulinzi wa rasilimali hizo kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
“Uhifadhi endelevu si kwa ajili ya wanyama pekee, bali ni msingi wa uchumi wetu na maendeleo ya jamii zetu,” alisema Dkt. Kijaji.
Katika kikao hicho, Waziri Kijaji aliahidi kuwa wizara itaendelea kushirikiana na viongozi wa jamii katika kulinda rasilimali za asili na kuimarisha ushirikiano kati ya serikali na wananchi ili kuzuia uharibifu wa mazingira na vitendo vinavyohatarisha ustawi wa maliasili.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Longido, Mhe. Thomas Ngobei, aliahidi ushirikiano wa dhati katika juhudi za uhifadhi hususan katika mchakato wa kuanzisha Hifadhi ya Jamii ya Ziwa Natron (JUHIZINA), akisisitiza kuwa jamii itaendelea kushiriki katika ulinzi wa mazingira kwa maslahi mapana ya taifa.

Katika hatua nyingine, Waziri Kijaji alikutana na uongozi wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) na kuwataka kuongeza kasi ya utekelezaji wa majukumu yao ili kufikia malengo ya serikali katika kukuza utalii na kuimarisha usimamizi wa hifadhi.
Kikao hicho kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, pamoja na wataalamu mbalimbali wa sekta hiyo.











