RIPOTA PANORAMA
MAWAKILI wa Kampuni ya Uwakili ya Haki Kwanza Advocates wanaomuwakilisha mchora katuni maarufu Afrika, Ally Masoud Nyomwa, maarufu zaidi kwa jina la Masoud Kipanya wameanza kuandaa mashtaka ya kumshtaki nayo mahakamani Burton Mwemba Mwijaku.
Akizungumza na waandishi habari Juni 15, mwaka huu katika ukumbi wa Hekima Garden, uliopo Mikocheni jijini Dar es Salaam, Wakili Mwandamizi wa Kampuni ya Uwakili ya Haki Kwanza Advocates, Alloyce Komba alisema yeye na mawakili wenzake wanakusudia kumshtaki mahakamani Mwijaku kwa kutumia ukurasa wake wa facebook na akaunti nyingine katika mitandao ya kijamii kusambaza waraka wenye maneno ya uongo ya kumkashfu Kipanya.
Komba alisema Juni 4, mwaka huu akitumia mitandao ya kijamii, Mwijaku alisambaza waraka kwenye mitandao ya kijamii bila sababu yoyote akieleza kuwa Kipanya anafanya biashara haramu ambayo imefanya vijana kuharibiwa maisha yao.
Kwamba siku hiyo, Mwijaku alitumia mitandao ya kijamii kusambaza waraka unaoeleza kuwa Kipanya huwazodoa viongozi wa nchi na marais kwa kuwadhalilisha na anakubali kutumika kwa kuhongwa ili kuisema vibaya serikali na viongozi wake.

Wakili Mwandamizi wa Kampuni ya Uwakili ya Haki Kwanza Advocates, Alloyce Komba
Alisema maneno hayo ya uongo na yenye nia ovu yanaendelea kuzunguka mitandaoni na kuifikia jamii ya watanzania wa ndani na nje ya nchi pamoja na jamii ya kimataifa hivyo kumshushia hadhi Kipanya.
Komba alisema Juni 7, 2024 aliagizwa na Kipanya kumwandikia Mwijaku notisi ya madai ya kumtaka ndani ya siku tatu akubali kuwa amesema uongo dhidi yake akiwa na nia ovu, aombe radhi kwa maandishi kwenye mitandao yote aliyotumia kueneza kashfa na maneno ya kutunga na pia akiri kumkosea Kipanya, jamii ya watanzania na dunia nzima kwa kuidanganya.
“Barua yetu ilibainisha kuwa endapo hatafanya hayo aliyoelekezwa, tumeagizwa kumfungulia mashtaka ya kashfa mahakamani na kumdai fidia ya Shilingi bilioni 5 kwa kumvunjia heshima Kipanya na pia kumshushia hadhi aliyoijenga kwa zaidi ya miaka 30 kitaaluma, kibiashara na jamii.

Masoud Kipanya
“Hadi leo, Mwijaku hajajibu kimaandishi yeye mwenyewe au kupitia kwa wanasheria wake hivyo Kipanya ametuagiza tuendelee na mchakato wa kumshtaki mahakamni ili hadhi yake irejeshwe na mahakama kutokana na athari alizopata na anazoendelea kuzipata,” alisema Wakili Komba.
Komba alisema yeye na mawakili wenzake wameanza kukusanya ushahidi kuhusu Kipanya kukashifiwa, kushushiwa hadhi na kuathirika kimaslahi, kijamii na kiheshima.