MAHAKAMA KUU YALIAMURU THE CITIZEN KUMLIPA MCHECHU BIL. 2.5

Date:

Share post:

RIPOTA PANORAMA

MAHAKAMA Kuu ya Tanzania imelihukumu Gazeti la The Citizen kumlipa aliyekuwa Mkurugenzi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Nehemia Mchechu Sh. bilioni 2.5 kwa kuandika habari iliyomchafulia jina lake.

Katika adhabu hiyo, Sh. bilioni 2 ni kwa ajili ya kumlipa fidia kwa kumchafulia jina alilolijenga kwa muda mrefu na kumshushia heshima na Sh. milioni 500 ni kwa ajili ya kumsababishia hasara ya jumla.

Mbali ya kiasi hicho cha fedha, Gazeti la The Citizen limeamuriwa kulipa gharama zote za uendeshaji wa kesi na kuandika habari ya kumwomba radhi katika ukurasa wake wa mbele kwa ukubwa ule ule na pia litalipa fidia asilimia 12 kila mwaka endapo litashindwa kulipa fedha hizo kwa wakati.

Katika hukumu hiyo, Mahakama Kuu pia imelionya Gazeti hilo kutomwandika tena Mchechu kwa habari ya uongo na yenye kumchafulia jina kiasi hicho isipokuwa pale tu kunapokuwa na ukweli na ushahidi wa kutosha.

Hukumu hiyo imetokana na kesi iliyofunguliwa na Mchechu dhidi ya Gazeti la The Citizen akiiomba mahakama iliamuru gazeti hilo limlipe fidia ya Sh. bilioni 3 na kumwomba radhi kwa madai ya kumchafulia jina na kushusha hadhi na heshima yake katika jamii.

Mchechu ambaye aliondolewa kwenye nafasi ya ukurugenzi wa Shirika la Nyumba la Taifa wakati wa Serikali ya Awamu ya Tano iliyokuwa chini ya Hayati Rais Dk. John Magufuli, alirejeshwa kwenye nafasi hiyo mwaka jana na Rais Samia Suluhu Hassan.

Hivi karibuni Rais Samia alimuhamisha Mchechu kutoka kwenye nafasi ya Mkurugenzi Mkuu wa NHC kwenda kuwa Msajili wa Hazina.

Machi 23, 201, Gazeti la The Citizen liliandika habari iliyobeba kichwa cha habari: “Why JPM dissolved NHC Board, Sacked Mchechu (Kwa nini JPM alivunja Bodi ya NHC na kumng’oa Mchechu?)

Habari hiyo iliyoainisha sababu kadhaa wa kadhaa kutoka vyanzo vyake mbalimbali zinazodaiwa kuwa sababu za Hayati Rais Dk. Magufuli, kuchukua uamuzi wa kuivunja Bodi ya NHC na kumwondoa Mkurugenzi Mkuu Mchechu. 

Baadhi ya tuhuma zilizoibuliwa kwenye habari hiyo ni pamoja na madai kwamba Mchechu alikuwa akichunguzwa na Bodi ya Wakurugenzi ya NHC na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kuhusu mgongano wa madaraka juu ya ununuzi wa ekari 500 za mradi wa NHC, Safari City, Arusha. 

Pia gazeti hilo lilidai kuwa Mchechu anachunguzwa na TAKUKURU kwa madai ya kumtumia mkandarasi aliyekodishwa na NHC kujenga barabara yake binafsi karibu na mradi huo wa NHC, Safari City. 

Kuhusu mradi wa Kawe, gazeti hilo lilidai kuwa Mchechu aliingia makubaliano  na kampuni ya ukandarasi ya PHILS International yenye makao yake Dubai, bila kushirikisha kitengo cha ununuzi cha NHC kinachoongozwa na Hamis Mpinda.

Hoja zingine zilizotajwa kwenye habari hiyo ni kuhusu madai kwamba Mchechu anachunguzwa kwa tuhuma kuwa kampuni ya mkewe ilipewa zabuni ya kutoa huduma za bima kwenye nyumba za NHC Mtwara, hali ambayo ni kinyume na maadili ya utumishi wa umma. 

Madai ya mwisho yaliyotajwa na gazeti hilo ni tuhuma za matumizi mabaya ya ofisi yaliyotajwa kwa kiwango kikubwa. 

HUKUMU

Akisoma hukumu hiyo, Jaji Leila alisema kuwa upande wa  mashitaka umeshindwa kuleta ushahidi kuthibitisha madai yao.

Alisema kuwa mahakama yake imeridhishwa na ushahidi uliotolewa na Mchechu kwamba habari iliyoandikwa dhidi yake ni ya uongo na ilikuwa na lengo la kumchafulia jina.

Alisema kuwa mashahidi wa upande wa Gazeti la The Citizen, Bernad James (Mhariri wa Habari za Mahakama) na Thomas Masyoba (Mhariri Mtendaji), walishindwa kuleta ushahidi kuthibitisha uhalali na usahihi wa habari hiyo.

“Mahakama inaheshimu vyanzo vya habari kama mashahidi walivyoeleza, lakini hakuna ushahidi wowote unaothibitisha. Kwa mfano mashahidi wanasema Mchechu alihojiwa  na TAKUKURU au Tume iliyoundwa kumchunguza, yeye anasema hajawahi kuhojiwa  na chombo chochote,” alisema Jaji Leila.

Alisema kuwa mashahidi wa upande wa mashitaka walisema habari yao ni mwendelezo wa kauli aliyoitoa Hayati Rais Dk. Magufuli wakati akifungua nyumba za NHC mjini Dodoma.

Alisema kuwa ushahidi wa video ya taarifa ya Hayati Rais Dk. Magufuli iliyorekodiwa na Kituo cha Televisheni cha Azam na kuonyeshwa hapa mahakamani, inaonyesha kuwa Hayati Rais Dk. Magufuli alisema kuna matumizi mabaya ya fedha ndani ya shirika hilo lakini hakumtaja mtu anayehusika.

“Lakini habari iliyoandikwa na Gazeti la The Citizen imeenda mbali na kuongeza mambo mengine ambayo Rais Magufuli hakuyasema na hayana ushahidi,” alisema Jaji Leila.

Jaji Leila alivitaka vyombo vya habari pamoja na taaluma zingine wakiwamo majaji kutimiza majukumu yao na kulinda haki na hadhi za wananchi bila kuwavunjia heshima katika jamii.

Alisema kuwa Mchechu ni mtu maarufu, mtumishi wa ngazi ya juu serikalini, yumo katika bodi mbalimbali na kiongozi wa kanisa hivyo kwenye ushahidi wake alisema habari hiyo ilimshushia hadhi na kulazimika kujiuzulu nafasi zake katika maeneo mengi aliyokuwa akiyatumikia.

Katika kesi hiyo, Mchechu alitetewa na mawakili Vitalis Peter na Aliko Mwamanenge wakati Gazeti la The Citizen lilitetewa na mawakili Ambrose Nkwera na Raban Rugina.

Awali katika utetezi wake, Mchechu alidai kuwa habari iliyochapishwa na gazeti hilo na kumhusisha na tuhuma za ubadhirifu na matumizi mabaya ya ofisi, imemshushia hadhi na heshima aliyoijenga kwa zaidi ya miaka 20 ndani na nje ya nchi.

Mchechu alidai kuwa habari hiyo ilikuwa ya uongo na yenye lengo la kumchafulia jina na kumvunjia heshima kwani wahusika hawakumhoji ili kuthibitisha madai hayo.

Alidai kuwa gazeti hilo liliandika habari hiyo, kuwa ameng’olewa kwenye nafasi yake na Hayati Rais Dk. Magufuli huku likijua fika kuwa hakung’olewa na Rais. 

Akifafanua hoja hiyo, Mchechu alidai kuwa alipewa likizo na hata wakati gazeti hilo linachapishwa alikuwa bado mfanyakazi wa NHC

“Mheshimiwa Jaji, liliandika habari hii likijua kuwa sijafukuzwa kwa kuwa nilikuwa sijafukuzwa kazi na wala Mheshimiwa Rais hakuwa na hakuwahi kunifukuza kazi.

 “Kwa hiyo hii ilikuwa ni habari ya uongo na yenye nia ovu ya kunichafua na kunishushia hadhi yangu katika familia, jamii, Taifa na duniani kwa ujumla,” alidai Mchechu. 

Kuhusu madai kuwa alihojiwa na TAKUKURU, Mchechu alidai hakuwahi kuhojiwa na chombo hicho wala chombo kingine chochote juu ya mgongano wa ununuzi wa ekari 500 za NHC kwa ajili ya mradi wa NHC Safari City. Katika tuhuma hiyo, Mchechu anadaiwa kuwa ndiye aliyewauzia NHC kiwanja hicho kwa bei kubwa zaidi kuliko bei halisi. 

Akitoa utetezi wake katika hilo, Mchechu alidai kuwa kwanza NHC haijawahi kununua ekari 500 Arusha na ukweli halisi ni kuwa NHC ilinunua ekari 583.

 “Binafsi sikuwahi kuhojiwa wala kuchunguzwa, iwe na Bodi au taasisi yoyote ya uchunguzi ikiwamo TAKUKURU juu ya ununuzi wa shamba la ekari 500 au lolote Arusha,” alidai Mchechu.

Mlalamikaji huyo alidai kuwa hajawahi kumiliki au kununua ardhi Arusha katika maisha yake yote na hata katika kampuni anazomiliki hazijawahi kumiliki au kununua ardhi Arusha.

“Na sijawahi kuiuzia NHC ardhi Arusha na pia mahali pengine popote Tanzania kabla sijawa mtumishi au nilipokuwa mtumishi katika uhai wa maisha yangu yote mpaka leo,” alidai Mchechu. 

Kuhusu madai kuwa anachunguzwa kwa kumtumia mkandarasi wa NHC kwa mradi wake binafsi, Mchechu alidai kuwa hajawahi kutumia mkandarasi yeyote wa NHC, hata asiye wa NHC kuandaa barabara katika ardhi yake binafsi, inayotajwa kuwa karibu na mradi wa Safari City kwa kutumia fedha za shirika hilo.

 “Na pia tofauti na tuhuma hii ukweli ni kuwa sina na sijawahi kuwa na ardhi karibu na mradi wa NHC Safari City na hata mkoa mzima wa Arusha katika maisha yangu yote,” alisisitiza.

Kuhusu mradi wa Kawe, Mchechu alidai kuwa hajawahi kukiuka taratibu za sheria ya ununuzi kuhusu mradi huo. 

“Kama ilivyo sheria ya ununuzi wa umma, uamuzi wa zabuni ya mradi wa Kawe huamuliwa na Bodi ya Zabuni ya Shirika. Sijawahi kukiuka taratibu za sheria ya ununuzi kwa kufanya au kupoka uamuzi wa Bodi ya Zabuni kwa mradi wa Kawe au mradi wowote ambao shirika lilifanya.

“Kwa maana hiyo, sikuwa na wajibu wa kumshirikisha aliyekuwa Mkuu wa Kitengo cha Ununuzi cha NHC, Hamisi Mpinda kwa jambo ambalo halikuwa katika uamuzi wangu,” alidai. 

Madai kuhusu kutumia kampuni ya mkewe kutoa huduma ya bima kwa nyumba za NHC Mtwara, Mchechu alidai kuwa shirika halikati bima kwa majengo yake bali hutumia mfuko maalumu wa pesa (Sinking Fund) kwa ajili ya bima ya majengo yake hivyo kampuni ya mkewe haijawahi kutoa huduma ya bima kwa NHC.

Akijibu madai ya matumizi mabaya ya ofisi Mchechu alidai hajawahi kuchunguzwa au kuitwa kuhojiwa na kamati yoyote, juu ya ukosefu wa maadili na matumizi mabaya wa fedha za umma. 

ATHARI

Mchechu alidai kuwa taarifa hiyo imemwathiri kwenye maeneo mengi katika maisha yake kwani iliwafikia watu wengi ndani na nje ya nchi. Alidai kuwa habari hiyo ilimsababishia mfadhaiko mkubwa wa akili, msongo wa mawazo, hofu na kudhuru afya yake.

 “Nilikosa kuaminika na hivyo kupoteza nafasi nyingi za kibiashara nilizokuwa nafanya na wenzangu wa kibiashara na kuondokewa na baadhi ya wabia katika kampuni ambazo nina uhusiano nazo kibiashara.

“Taarifa hii iliathiri hata kuaminika kwa taasisi niliyokuwa naiongoza na hivyo kuathiri ufanisi na utendaji wake wa kazi na kuaminika kwake kwa wateja,” alisema. 

Mbali na kuwa Mkurugenzi wa NHC, Mchechu kwa sasa pia ni Mwenyekiti wa Benki ya BOA, Mwenyekiti wa Kampuni za Amboni Group of Companies, Amboni Beach Properties na Amboni Sisal Limited. 

Pia Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa TANESCO, TANTRADE, TMRC, Kampuni ya Watumisihi Housing, mjumbe wa Bodi ya Chuo Kikuu cha Tumaini Tawi la Dar es Salaam, Katibu wa Usharika wa Kanisa la KKKT, Usharika wa Mbezi Beach na pia Mwenyekiti wa Halmashauri ya Fedha na Mipango wa Dayosisi ya Mashariki na Pwani (DMP) kama sehemu tu ya majukumu yake. 

About The Author

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

spot_img

Related articles

USIYOYAJUA KUHUSU KOCHA ALIYEANDIKA HISTORIA BUNDESLIGA

MUNICH, Ujerumani JINA la Marie-Louise Eta limeandika historia katika soka la Ujerumani baada ya kuwa mwanamke wa kwanza kuwa...

BURNA BOY HATAKI MAZOEA, ‘BIFU’ KWAKE KAWAIDA TU

HIVI karibuni, supastaa wa muziki wa Afrobeat, Burna Boy, aliingia kwenye mikono ya Chama cha 'Ma-dj' nchini Nigeria,...

BURKINA FASO IKO HOI AU HAI CHINI YA KAPTENI TRAORE?

HATUA ya kutangaza kuwa raia wake waaitarajie demokrasia imeibua maswali mengi juu ya uongozi wa Kapteni Ibrahim Traore...

SIMU YAKO CHANZO CHA UGONJWA WA MOYO, SARATANI?

UKWELI ulio wazi ni kwamba matumizi ya simu za mkononi yameongezeka kwa kasi duniani, Tanzania ikiwa na 'laini'...