UKIFUATILIA msimamo wa Ligi Kuu Bara na kiwango cha Simba katika mechi za hivi karibuni, unaweza kusema sasa kocha raia wa Afrika Kusini, Steve Barker, ameshaanza kulizoea soka la Tanzania.
Barker akitokea kwao, Afrika Kusini, alitua Bongo na kuikuta Simba inachechemea katika nafasi ya tano kwenye msimamo, ikiwa imekusanya pointi 12 pekee.
Kwamba Barker amechangia pointi 34 kati ya hizi 46 walizonazo sasa, pia Simba ikifunga mabao 21 na kuruhusu sita tu katika mechi 15 za Ligi alizokaa kwenye benchi la ufundi.
Tujikumbushe; mechi yake ya kwanza ilikuwa Januari 18, 2026, ambapo hata hivyo haikuwa na matokeo mazuri kwani Simba ililazimishwa sare ya bao 1-1 na Mtibwa Sugar.
Si tu matokeo yasiyoridhisha, pia wakati huo mashabiki hawakuwa wakifurahishwa na aina ya soka lililokuwa likichezwa na timu yao.
Taratibu, mambo yalianza kubadilika. Simba ikashinda mechi tatu mfululizo zilizofuata dhidi ya Mashujaa, KMC na Prisons, kila moja ikipata ushindi wa mabao 2-0.
Hata hivyo, mechi mbili zilizofuata mambo yaliharibika tena, ambapo Simba iliambulia suluhu (0-0) mbele ya Dodoma Jiji na Yanga.
Lakini, Simba ilirejea kwenye mstari kwa ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Singida Black Stars, kabla ya sare ya bao 1-1 ilipokutana na Pamba Jiji.
Matokeo hayo yalifuatiwa na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Coastal Union, kisha suluhu mbili mfululizo mbele ya Azam na TRA United.
Mchezo huo ulifuatiwa na ushindi mnono katika mechi mbili mfululizo dhidi ya Fountain Gate (3-0) na Namungo (3-1), sare ya 2-2 dhidi ya Yanga, na ushindi wa bao 1-0 mbele ya JKT Tanzania.






