RAIA WA AFRIKA KUSINI NA CHUKI DHIDI YA WAGENI; CHANZO NA MADHARA YAKE

Date:

Share post:

JOHANNESBURG, Afrika Kusini
SIKU za hivi karibuni yameshuhudiwa matukio ya vurugu zinazofanywa na baadhi ya wananchi wa Afrika Kusini dhidi ya raia wa kigeni.

Chuki dhidi ya wageni zimekuwa zikihusisha uharibifu wa mali zao, kujeruhiwa na hata kuuawa kwa vipigo.

Ikumbukwe, Afrika Kusini ina raia wa kigeni milioni 2.4, kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2022.

Video mbalimbali zilizosambaa kwenye majukwaa ya kidigitali zinawaonesha raia hao wa Afrika Kusini wakiwa na silaha za jadi, yakiwamo mapanga.

Waathirika wakubwa wa matukio hayo ni raia wa kigeni wanaotoka mataifa ya Ghana, Zimbabwe na Nigeria, ambao kimsingi ndiyo wengi zaidi nchini Afrika Kusini.

Kwa upande mwingine, hii si mara ya kwanza kwa Afrika Kusini, hasa miji mikubwa ya Johannesburg na Cape Town, kugubikwa na matukio ya aina hii, na badala yake yamekuwa yakiibuka na kupotea.

Wazawa wanaofanya vitendo hivyo wamekuwa na madai wanayoyaita ya msingi, kwamba wageni wamekuwa wakichukua ajira zao.

Pia, mbali ya wazawa kudai wingi wa wageni umesababisha kudorora kwa hudma za kijamii, pia wanawataja kuongeza kiwango cha matukio ya uhalifu nchini kwao.

Kwa upande wao, wachambuzi wa siasa za Afrika wanaiona hatari ya vitendo hivyo kuathiri uhusiano wa Afrika Kusini na mataifa mengine, hasa yenye raia wake wengi nchini humo.

Mathalan, Serikali za Ghana, Zimbabwe na Nigeria zimelaani vurugu dhidi ya raia wake, zikizitaka mamlaka za Afrika Kusini kuchukua hatua za haraka.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ghana, Samuel Okudzeto Ablakwa, alieleza kusikitishwa na moja ya video ya raia wake anayeishi KwaZulu-Natal, Afrika Kusini.

Katika video hiyo, kundi la vijana wa Afrika Kusini wanaonekana wakimshambulia, huku wakimtaka kuondoka nchini humo na kurudi kwao (Ghana).

Ablakwa anasema viongozi wa harakati za kupigania uhuru wa Afrika Kusini chini ya Chama cha African National Congress (ANC) walipewa hifadhi na mataifa ya Afrika walipokimbia hila za wakoloni wakati wa sera ya ubaguzi wa rangi.

Hivyo, Ablakwa anaitaka ANC, ambayo sasa iko madarakani ikiiongoza Afrika Kusini, kuhakikisha inawalinda raia wa kigeni dhidi ya chuki za wazawa.

Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa, naye amelaani vitendo vya chuki dhidi ya raia wa kigeni, huku akiwataka kuheshimu sheria kwa kuepuka kujihusisha na uhaifu.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

spot_img

Related articles

NAMIBIA YA MALIZA DENI LA IMF

Rais wa Namibia, Netumbo Nandi-Ndaitwah, ameiongoza nchi yake kufikia hatua muhimu ya kiuchumi baada ya kukamilisha malipo yote...

SERIKALI KUONGEZA UWEKEZAJI KWA WAKUNGA KUIMARISHA AFYA YA MAMA NA MTOTO NCHINI

Serikali kupitia Wizara ya Afya imejipanga kuendelea kuongeza uwekezaji katika mafunzo, ajira, motisha na mazingira ya kazi kwa...

POLISI KUENDELEA KUDHIBITI WAZUSHI MITANDAONI, LIKIIMARISHA ULINZI KUELEKEA DERBY YA SIMBA NA YANGA

Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limetoa taarifa ya matukio mbalimbali ya kiusalama na kisheria,...

DKT. SAMIA AFANYA UTEUZI, UTENGUZI NA UHAMISHO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amefanya uteuzi na uhamisho wa baadhi...