​Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza limewafikisha mahakamani watu wawili wanaotuhumiwa kwa makosa ya jinai yanayohusiana na dawa za kulevya.

​Washtakiwa hao, Madumuka Zilihona (60) na Mawazo Manisha (50), wakulima na wakazi wa kijiji cha Busekeseke Wilayani Sengerema, wamepandishwa kizimbani Juni 23, 2026, katika Mahakama ya Wilaya ya Sengerema ambapo mmoja amesomewa mashtaka mawili na mwingine shitaka moja.

​Mshtakiwa wa kwanza, Madumuka Zilihona, amesomewa makosa mawili mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Magreth Maruma.

Wakili wa Serikali, Rivona Kasinisala amedai kuwa ​kosa la kwanza linalomkabili Madumuka ni kukutwa na dawa za kulevya kinyume na kifungu namba 15 (1)(a) na (3)(iii) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Sura ya 95 Marejeo ya mwaka 2023, ikisomwa pamoja na aya ya 23 ya jedwali la kwanza na vifungu vya 57(1) na 61(2) vya Sheria ya Udhibiti wa Makosa ya Uhujumu Uchumi na Uhalifu wa Kupangwa, Sura ya 200 Marejeo ya mwaka 2023.

Kutokana na mahakama hiyo kutokuwa na mamlaka kisheria ya kusikiliza shauri hilo, ​mshitakiwa hakutakiwa kujibu chochote kuhusiana na kosa, huku pia mahakama ikimuamuru kuendelea kubaki mahabusu hadi upelelezi utakapokamilika.

​Kosa la pili ni kulima mimea isiyoruhusiwa kinyume na kifungu namba 11(1)(a) na (d) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya Sura ya 95 toleo la mwaka 2023.

Shitaka la pili, imedaiwa na Wakili wa Serikali Rivona Kasinisala kwamba mshitakiwa Madumuka Zilihona mnamo Mei 23 2026, katika kata ya Kalebezo Wilayani Sengerema Mkoani Mwanza alikutwa anamiliki ekari mbili za mimea isiyoruhusiwa aina ya bangi.

​Mshtakiwa wa Pili, Mawazo Manisha, anadaiwa kwamba Mei 23, 2026 katika kitongoji cha Barabara ya Nyerere iliyopo Kijiji cha Busekeseke Wilayani Sengerena alikutwa na dawa za kulevya zenye uzito wa kilo 13.50 kinyume na Kifungu namba 16(1) na (2)(c) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Sura ya 95 toleo la mwaka 2023.

​Mshtakiwa huyo alikana shtaka hil ambapo Hakimu Mkazi Mwandamizi Magerth Maruma alieleza kuwa kosa hilo lina dhamana na kuweka masharti kwamba mshtakiwa anapaswa kuwa na wadhamini wawili watakaosaini dhamana ya Shilingi milioni 4 kila mmoja, wawe na vitambulisho vinavyotambulika pamoja na barua za utambulisho kutoka Serikali za Mitaa.

Hata hivyo, mshtakiwa alishindwa kukidhi vigezo hivyo vya dhamana na kurudishwa rumande hadi Julai 2, 2026.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here