Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema Serikali imeanza kulipa malimbikizo ya madeni ya watumishi inchini yakiwemo ya hifadhi ya jamii, posho za likizo, uhamisho na mishahara, huku akiahidi ulipaji huo utaendelea kufanyika kwa awamu kulingana na tathmini inayoendelea.
Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani(Mei Mosi) yaliyofanyika kitaifa mkoani Njombe, Rais Samia amesema Serikali ya awamu ya sita imeendelea kuweka mikakati madhubuti ya kuboresha maslahi ya wafanyakazi na kuimarisha ustawi wao.
Katika sekta ya ajira, Rais Samia amesema Serikali imefanikiwa kuratibu fursa za ajira nje ya nchi ambapo vijana 7,593 tayari wamenufaika, huku juhudi zaidi zikiendelea kupunguza tatizo la ajira kwa vijana nchini.
Aidha, amebainisha kuwa licha ya changamoto za kiuchumi zinazoikumba dunia, Serikali inaendelea kuchukua hatua kuhakikisha Watanzania wanabaki na hali nzuri ya maisha au kuiboresha zaidi, akisisitiza kuwa ugumu wa hali ya uchumi huanza kubebwa na Serikali kabla haujafika kwa wananchi.
Kuhusu mishahara, Rais Samia amesema asilimia 80 ya waajiri wa sekta binafsi wameanza kulipa kima cha chini cha mshahara cha shilingi 358,322, huku Serikali ikiendelea kufanya mazungumzo na waliobaki ili kufikia utekelezaji kamili.
Hatahivyo Rais Samia Amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kazi na maslahi ya watumishi kadri hali ya uchumi itakavyoruhusu, huku akiwahimiza wafanyakazi kuendelea kufanya kazi kwa bidii, nakuwaeleza kuwa Serikali inawasikiliza na kuthamini mchango wao katika maendeleo ya taifa.






