MANCHESTER, Uingereza
MMILIKI wa klabu ya Manchester City, Sheikh Mansour bin Zayed Al-Nahyan, anakabiliwa na tuhuma nzito za kusambaza silaha zinazotumika kwenye machafuko yanayoendelea nchini Sudan.
Taasisi ya Haki za Binadamu ya FairSquare imeitaka Serikali ya Uingereza kuchunguza uhusiano uliopo kati ya Zayed Al-Nahyan na wapiganaji wa Sudanese Rapid Support Forces (RSF) wanaoshutumiwa kwa uhalifu wa kivita.
Marekani na Uingereza zimekuwa zikiwawekea vikwazo watu waliobainika kuwa na ukaribu na RSF na sasa wanaharakati wanataka Sheikh Mansour naye ashughulikiwe.
NI MTU WA AINA GANI?
Ifahamike kuwa mbali ya soka, ambapo ameifanya Man City kuwa moja ya klabu kubwa za soka barani Ulaya, pia Sheikh Mansour ni kiongozi wa Taifa la Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).
Wachambuzi wa siasa wanamtaja Sheikh Mansour kuwa ndiye injini ya UAE, hasa katika mipango thabiti ya kiusalama, vita na hata kiuchumi.
Si tu haonekani hadharani mara kwa mara, kama ambavyo amekuwa akihudhuria mechi chache cha Man City, ni nadra pia kuzungumza kwenye vyombo vya habari.
Hata hivyo, tabia yake ya kukwepa mikutano mingi ya kidiplomasia inatafsiriwa kuwa ni njia ya kukimbia tuhuma nyingi zinazomkabili.
HOJA YA WANAHARAKATI
Wanaharakati wa haki za binadamu wa FairSquare wanasema: “Kuna ushahidi wa kutosha kutoka katika vyanzo vya kuaminika, ikiwamo timu ya wataalamu ya Umoja wa Mataifa, kuthibitisha kuwa UAE imekuwa ikiisapoti RSF kwa silaha na huduma zingine tangu Juni, 2023.
“Ni kinyume cha tamko la Umoja wa Mataifa la mwaka 2024. Kwa kufanya hivyo, UAE imechangia ongezeko la mgogoro Sudan …”
Pia, ka mujibu wa wanaharakati hao, UAE imekuwa kambi ya watu au taasisi kukutana na kusuka mipango ya kuisaidia RSF.
TATIZO LILIANZIA HAPA
Aprili, 2023, wiki chache tu kabla ya vita vya wenyewe kwa wenyewe kuanza nchini Sudan, taarifa zinasema Sheikh Mansour alikutana na kiongozi wa RFS, Mohamed Hamdan Dagalo ‘Hemeti’.
Taarifa zinaeleza kuwa ajenda ya mazungumzo ilikuwa ni namna UAE itakavyowasaidia wapiganaji wa RFS.
Baadaye, UAE ilionekana kuwa mstari wa mbele katika kutoa misaada nchini Sudan, ingawa Marekani inaanini kilikuwa ni kivuli cha kupitisha silaha, zikiwamo ndege zisizo na rubani, kwa Hemeti na watu wake.
SHUTUMA ZINGINE ZINAZOMKABILI
Sheikh Mansour pia anahusishwa na machafuko yanayoendelea nchini Libya, akitajwa kumfadhili Jenerali Khalifa Haftar tangu mwaka 2015.
Mwaka 2023, Serikali ya Uingereza ilimgomea alipotaka kununua Gazeti maarufu la Daily Telegraph kutokana na kashfa kubwa ya rushwa iliyokuwa ikimkabili wakati huo.
Kashfa ya 1MDB, ambapo kupitia kampuni zake, Sheikh Mansour alitajwa kuwa sehemu ya vigogo waliochota mabilioni ya fedha katika Serikali ya Malaysia.
Klabu yake ya Man City pia inachunguzwa kwa makosa zaidi ya 100, yakiwamo ya kukiuka nidhamu ya utumizi wa fedha katika uendeshaji wake.






