Sunday, June 15, 2025
spot_img

JESHI LA POLISI KUENDELEA KUSHIRIKIANA NA RSA TANZANIA KUIMARISHA USALAMA BARABARANI

Jeshi la Polisi nchini limesema linatambua mchango mkubwa unaotolewa na asasi ya Mabalozi wa Usalama Barabarani (RSA) Tanzania katika kuimarisha usalama barabarani huku likiahidi kuendelea kushirikiana na mabalozi katika kufanikisha jukumu la kuimarisha usalama barabarani.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa kipolisi wa Kinondoni Mrakibu Mwandamizi wa Polisi Solomoni Mwangamilo, wakati wa kikao cha wadau wa usalama barabarani kilichoandaliwa na RSA Tanzania kwa ajili ya kutambulisha na kujadili dhana mpya ya Ukanda wa Spidi 30 (30KpH Zones) katika maeneo ya makazi kama njia ya kuwalinda watumia barabara.

Afande Solomoni amesema kwamba mtandao mpana wa mabalozi wa usalama barabarani umekuwa na msaada mkubwa sana kwa Jeshi kwani kuna nyakati wamekuwa wakipata taarifa za awali za ajali kutoka kwa mabalozi jambo ambalo limesaidia Kikosi kuweza kushughulikia matatizo hayo kwa haraka zaidi.

“RSA Tanzania imekuwa taasisi ya mfano katika kusaidia juhudi za Kikosi na Taifa letu za kuimarisha usalama barabarani, sisi katika Kikosi cha Usalama Barabarani tunatambua na kuthamini mchango wao mkubwa kwani wamekuwa chanzo cha kuaminika cha taarifa na matukio ya ajali kwetu sisi, na hiyo imesaidia Kikosi kushughulikia matatizo hayo haraka yanapotokea” amesema Afande Solomoni.

Kuhusu mradi wa 30KpH, afande Solomoni ambaye pia ni Katibu wa Kamati ya Usalama Barabarani Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni amesema;

“Serikali imeboresha barabara nyingi za kwenye maeneo ya makazi, bahati mbaya maboresho haya yamegeuka chanzo cha majonzi na vilio kutokana na baadhi ya madereva kugonga na kuua au kujeruhi watu kwa kukimbiza magari, hivyo utekelezaji wa dhana hii ya 30KpH, utasaidia sana kuimarisha ustawi wa jamii zetu huko mitaani”

Aidha Afande Solomoni amesema kwamba Kikosi kitakuwa tayari kuendelea kushirikiana na RSA Tanzania kwa kupokea taarifa na ushauri wao na kuufanyia kazi pamoja na kushirikiana nao katika kufanikisha juhudi zozote zenye lengo la kuimarisha usalama barabarani.

Baadhi ya wadau walioshiriki kikao hicho wamesema pamoja na utekelezaji wa dhana ya 30KpH kuwa itasaidia sana kupunguza ajali za watembea kwa miguu kugongwa, ipo haja ya serikali kushauriwa kuhakikisha barabara zote zinazojengwa zinakuwa na sehemu rasmi za watembea kwa miguu ili kuwazuia wasiingie barabarani.

Akiwasilisha mada katika kikao hicho, Mtendaji Mkuu wa RSA Tanzania balozi Augustus Fungo, alisema kwamba dhana ya 30KpH, ni dhana iliyofanyiwa utafiti na wataalamu wa masuala ya usalama barabarani na kubainika kwamba sio tu itasaidia kupunguza ajali za watembea kwa miguu kugongwa, bali pia itasaidia kurahisisha utembeaji wa magari na hivyo kupunguza kadhia za foleni.

Aliongeza kwamba licha ya baadhi ya madereva kuonyesha dalili za kuipinga wakisema itachangia safari kuzidi kutumia muda mrefu na kuwachosha madereva, ukweli ni kwamba dhana hiyo haijalenga kabisa barabara kuu bali barabara za mitaa ambako ni makazi ya watu.

Kikao hiki kilifanyika kama sehemu ya utekelezaji wa mradi wa uhamasishaji wa “Dhana ya Ukanda wa Spidi 30” unaofadhiliwa na Shirika la Kimataifa la Global Alliance of NGOs for Road Safety na unatekelezwa nchini na asasi ya Mabalozi wa Usalama Barabarani

Nyingine Zinazohusiana na Hii

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Tufuatilie

0FansLike
3,913FollowersFollow
0SubscribersSubscribe
- Advertisement -spot_img

Habari Nyingine Mpya