Rais wa Vladimir Putin ameahidi kulipiza kisasi dhidi ya Ukraine baada ya kuishutumu kwa kufanya shambulio baya lililolenga bweni la wanafunzi katika eneo linalokaliwa na Urusi mashariki mwa Ukraine.
Kwa mujibu wa Putin, watu sita waliuawa huku wengine 39 wakijeruhiwa kufuatia shambulio la usiku kucha lililotokea katika mji wa Starobilsk, mkoa wa Luhansk. Aidha, watu wengine 15 wanadaiwa kutoweka baada ya tukio hilo.
Jeshi la Ukraine limethibitisha kufanya shambulio dhidi ya makao makuu ya kikosi maalumu cha kijeshi cha Rubicon kilichopo Starobilsk, lakini halikubainisha iwapo jengo hilo ndilo lililoripotiwa kushambuliwa na Urusi.
Akizungumza katika makazi yake ya Kremlin siku ya Ijumaa, Putin alisema eneo lililoshambuliwa halikuwa na vituo vya kijeshi wala huduma za kijasusi, akisisitiza kuwa hakuna msingi wa kudai kuwa mfumo wa ulinzi wa anga wa Urusi ulihusika na tukio hilo.
Kiongozi huyo wa Urusi pia alisema shambulio hilo lilifanywa kwa kutumia ndege zisizo na rubani 16 zilizorushwa kwa awamu tatu tofauti. Kufuatia tukio hilo, ameagiza jeshi la Urusi kuandaa mapendekezo ya namna ya kujibu mashambulizi hayo.
Televisheni ya serikali ya Urusi ilimuonyesha mmoja wa majeruhi waliokuwa wakipatiwa matibabu, aliyetambulika kwa jina la Diana Shovkun mwenye umri wa miaka 19.







