Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) limethibitisha kifo cha baharia raia wa Tanzania, Mchama Maregesi Mongu, aliyefariki dunia Mei 3, 2026 wakati akitekeleza majukumu yake katika meli ya kuvuta (tug boat) iitwayo VOLANS.
Kwa mujibu wa taarifa ya TASAC, meli hiyo iliyosajiliwa na Shirika la Usajili la Kimataifa wa Bahari (IMO Na. 9298566) na kubeba bendera ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), iliyokuwa ikisafiri kutoka UAE kuelekea Oman kabla ya kushambuliwa na bomu wakati ikipita katika Mfereji wa Hormuz, eneo linalounganisha nchi za Iran na Oman.
TASAC imetoa pole kwa familia, ndugu na marafiki wa marehemu kufuatia msiba huo mzito, huku ikiungana nao katika kipindi hiki cha majonzi.
Aidha, shirika hilo limesema linaendelea kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kufuatilia kwa karibu tukio hilo, ikiwa ni pamoja na juhudi za kuurejesha mwili wa marehemu nchini mara utakapopatikana.
Katika hatua nyingine, TASAC imekumbusha umuhimu wa kulinda maisha ya mabaharia wanaofanya kazi katika maeneo hatarishi, ikisisitiza uzingatiaji wa haki ya kupita kwa amani (innocent passage) kwa mujibu wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Sheria za Bahari (UNCLOS).






