Rais wa William Ruto amesema nchi za Afrika Mashariki zina fursa kubwa ya kuongeza biashara ya ndani na kunufaika zaidi kiuchumi iwapo zitaimarisha ushirikiano wa kikanda.
Akilihutubia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini Dodoma leo Mei 5, 2026, Ruto amesema kiwango cha biashara ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki bado ni kidogo, kikikadiriwa kuwa kati ya asilimia 15 hadi 30, hali inayoonyesha kuwa sehemu kubwa ya biashara inaendelea kufanyika nje ya ukanda huo.
Aidha ameongeza kuwa pamoja na changamoto hiyo, bado kuna fursa kubwa kwa nchi wanachama kuongeza biashara baina yao, hatua itakayosaidia kufungua masoko mapya, kuimarisha viwanda na kuongeza ajira kwa wananchi.
Rais Ruto amesisitiza kuwa vijana ndio chachu ya mafanikio ya ajenda hiyo, akieleza kuwa kila mwaka mamilioni ya vijana kutoka nchi za ukanda huo wanaingia kwenye soko la ajira wakiwa na vipaji, na ndoto kubwa ambapo vijana hao hawahitaji misaada bali wanahitaji fursa, akibainisha kuwa kwa kuimarisha ushirikiano wa kikanda, kuwekeza katika miundombinu ya pamoja na kupanua biashara, Afrika Mashariki inaweza kuwa kinara wa ajira, ujasiriamali na maendeleo endelevu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.






