Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, amesema Serikali imeweka mkazo katika kuimarisha matumizi ya Kiswahili katika michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) kwa kuandaa Istilahi maalumu 420 zitakazotumika katika shughuli mbalimbali za mashindano hayo.
Akiwasilisha bajeti ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma leo Mei 4, 2026, Waziri Makonda amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha Kiswahili kinatumika kwa ufasaha katika mawasiliano ya kimataifa kupitia michezo.
Aidha Ameeleza kuwa Istilahi hizo zimeandaliwa kwa ushirikiano na wataalamu wa lugha na taasisi husika ili kuendana na mahitaji ya kimataifa ya utangazaji, uandishi wa habari na mawasiliano ya michezo.
Sanjari na hayo Makonda amesema mpango huo pia ni sehemu ya kuendeleza hadhi ya Kiswahili kama lugha ya Afrika na dunia, hasa Tanzania ikiwa miongoni mwa wenyeji wa AFCON 2027.
Mbali na hayo Ameongeza kuwa Serikali itaendelea kuimarisha matumizi ya Kiswahili katika sekta zote ili kukifanya kiwe na ushindani zaidi katika anga la kimataifa.






