SHIRIKA la Hifadhi za Taifa (TANAPA), kwa kushirikiana na wadau wa utalii na uhifadhi, wamefanya mazoezi ya pamoja (jogging) Aprili 8, 2026 katika Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro ikiwa ni maandalizi ya msimu wa tatu wa tamasha la utalii la Same Utalii Festival.
Tamasha hilo linatarajiwa kufanyika kwa siku tatu kuanzia Aprili 10 hadi 12, 2026, likiwa na lengo la kuwakutanisha Watanzania na wageni mbalimbali kutembelea vivutio vya utalii na kuangazia fursa za uwekezaji zilizopo wilayani humo.
Akizungumza katika tukio hilo, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Same, Yusto Mapande, amesema lengo ni kuifanya Same kuwa kitovu cha utalii mkoani Kilimanjaro na miongoni mwa maeneo yanayoongoza kitaifa kwa mchango wa sekta hiyo katika uchumi.
Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Ninzari Iddi, amewahimiza wananchi kushiriki mazoezi ya mwili ili kuboresha afya na kujikinga na magonjwa yanayozuilika.
Kwa upande wake, Mhifadhi Mwandamizi kutoka Hifadhi ya Taifa Mkomazi, Geofrey Kyando, amesema tamasha hilo lina kaulimbiu “Same Utalii Festival, Make Same Green,” inayolenga kuhamasisha utunzaji wa mazingira na uhifadhi wa viumbe hai.
Tamasha hilo lilianza mwaka 2024 na sasa linafanyika kwa msimu wa tatu, likitarajiwa kujumuisha ziara katika vivutio kama Msitu wa Shengena na Mlima Kidenge.












