ISLAMABAD, Pakistan
WAZIRI Mkuu wa Pakistan, Muhammad Shehbaz Sharif, ametangaza kuwa nchi yake itakuwa mwenyeji wa mazungumzo ya amani kati ya Marekani na Iran.
Sharif amesema Pakistan iko katika maandalizi ya kuwapokea wawakilishi wa mataifa hayo, ambao wanatarajiwa kukutana Ijumaa ya wiki hii.
Kupitia ukurasa wake wa mtandao wa X, Sharif amesema kuwa Jamhuri ya Iran na Marekani, pamoja na washirika wao, wamekubaliana kusitisha mapigano yote, ikiwamo yale yaliyokuwa yakiendelea nchini Lebanon na maeneo mengine.
“Nina furaha kutangaza kuwa Jamhuri ya Iran na Marekani, sambamba na washirika wao, wamekubaliana kusitisha mapigano yote,” ameandika.
Aidha, ameeleza kuwa ana matumaini makubwa kuwa mazungumzo hayo yataleta matokeo chanya katika kumaliza mgogoro unaoendelea Mashariki ya Kati.
Awali, Rais wa Marekani, Donald Trump, alitangaza kuwa wamefikia makubaliano na Iran ya kusitisha mapigano kwa muda wa wiki mbili.
Imeandaliwa na Hassan Mwasha

