Klabu ya Tottenham Hotspur imepiga hatua kubwa katika harakati za kumsajili Sávio Moreira de Oliveira kutoka Manchester City wakati wa dirisha hili la usajili.
Kwa mujibu wa taarifa zilizochapishwa na Fabrizio Romano, mazungumzo kati ya pande husika yanaendelea vizuri huku Savinho akionekana kuwa tayari kuhamia Tottenham.
Winga huyo wa kimataifa wa Brazil amekuwa akifuatiliwa na Spurs kwa muda mrefu tangu msimu uliopita.
Inaelezwa kuwa Tottenham tayari wanafanya mazungumzo kuhusu masuala binafsi ya mchezaji huyo na wana matumaini makubwa ya kufanikisha usajili huo.
Kwa upande mwingine, Manchester City haina pingamizi la kumuuza Savinho ikiwa itapokea ofa itakayoridhisha.
Savinho, ambaye anajulikana kwa kasi, uwezo wa kupiga chenga na kutengeneza nafasi za mabao, anaonekana kuwa mmoja wa wachezaji wanaolengwa kuimarisha safu ya ushambuliaji ya Tottenham kuelekea msimu mpya.
Hata hivyo, hadi sasa hakuna makubaliano rasmi yaliyotangazwa, na mazungumzo yanaendelea kati ya klabu hizo mbili huku mashabiki wakisubiri kuona hatma ya nyota huyo wa Brazil.







